PAUL Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam amesema, kama isingekuwa njaa, basi angefanya uamuzi wa kujiuzulu nafasi hiyo baada ya kukosolewa na Rais John Magufuli. Anaripoti Martin Kamote … (endelea).
Amesema, aliona haya pale Rais Magufuli alipomkosoa kuhusu kusuasua kwa miradi ya ujenzi wa Machinjio ya Vingunguti na Fukwe ya Coco Beach.
Akizungumza katika hafla ya kuwadhamini wanafunzi 100 wa Kidato cha IV mchepuo wa Sayansi, wanaotoka katika familia masikini leo tarehe 17 Septemba 2019 jijini Dar es Salaam, Makonda amesema, njaa ndio iliyomfanya asijiuzulu.
Makonda ameeleza, kauli hiyo iliyotolewa na Rais Magufuli jana tarehe 16 Septemba 2019, ilikuwa ni aibu na kuwa kama asingekuwa na njaa kali, leo angandika barua ya kujiuzulu.
Aidha, Makonda amedai kwamba kuna baadhi ya wanasiasa jijini humo wanakwamisha utekelezwaji wa miradi kadhaa, wakitaka kupatiwa rushwa.
Kufuatia changamoto hiyo, Makonda amesema anaunda kamati maalumu kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika mkoa wa Dar es Salaam. Wajumbe watakaokuwa katika Kamati hiyo ni pamoja na maafisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU).
Leave a comment