PAUL Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania ametoa saa 24 kwa wabunge waliopo jijini humo kurudi Dodoma kuhudhuria vikao vya Bunge lasivyo watakamatwa kama kama wazururaji wengine. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam…(endelea)
Makonda ametoa kauli hiyo leo tarehe 6 Mei 2020 akisema atawakamata wabunge wote waliopo Dar es Salaam bila kibali cha Spika wa Bunge.
“Hakuna asiyefahamu kuwa sasa hivi tuko katika mapambano dhidi ya virusi vya Corona na sio uzururaji, ifahamike huu sio mji wa wazururaji hivyo natoa saa 24 kwa wabunge wote kurudi Dodoma tofauti na hapo tutawakamata kwa kosa la uzururaji kama tunavyowakamata machangudoa,” amesema Makonda.
Makonda amesema wabunge hao hawawatendei haki wananchi kwa sababu wanakwepa mjadala wenye maslahi kwao wa bajeti ya kuu ya serikali yam waka 2020/21. Amesema wabunge hao wamekimbilia jijini Dar es Salaam kwa lengo la kustarehe.
Baada ya kauli hiyo baadhi ya wabunge wamezungumzia agizo hilo akiwamo Mbunge wa Kigoma Mjini kupitia ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ambaye ametumia ukurasa wake wa Twitter akisema, “mimi ni Mbunge wa Kigoma Mjini.
https://www.youtube.com/watch?v=xRscCGp-6kE
Nipo Dar es Salaam sijakwenda Dodoma bungeni kwa sababu ninaamini kuwa Bunge lilipaswa kuahirishwa ili kupambana na Corona.”
“Sitakwenda Dodoma, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam hana mamlaka yoyote ya kuniamulia niwe wapi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Zitto ambaye pia ni Kiongozi wa ACT-Wazalendo
Naye Ester Bulaya, Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ambaye pia ni mbunge wa Bunda Mjini kupitia Chadema ameandika kwenye akaunti yake ya Twitter akisema, “…usitafute kiki kupitia sisi, sisi tupo karantini tunajitambua, utaishia kukamata wabunge wa chama chako na mawaziri wenu ambao hawatulii Dodoma, anza na waziri wa afya si anakuwaga Dar kamata kama mzururaji acha kujitutumua.”
Leave a comment