PAUL Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ameelezea namna alivyoupokea msiba wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba, akisema kuwa ulimpa wakati mgumu. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Makonda ametoa kauli hiyo wakati akizungumza katika shughuli ya kuuaga mwili wa Ruge iliyofanyika leo tarehe 2 Machi 2019 kwenye viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Makonda amesema wakati anajadiliana na familia ya marehemu Ruge kuhusu nafasi ya yeye kutoa salamu za rambirambi, alikuwa na wakati mgumu sana kutokana na kutokuwa na neno la kusema kuhusu msiba huo.
“Jana wakati tunajadiliana habari ya kutoa salamu za rambirambi kwangu nilikuwa na wakati mgumu sana, wakati mgumu sababu Ruge alikuwa zaidi ya rafiki kwangu. Familia yake ilijua jinsi tulivyokuwa karibu, na hata mambo ambayo hayakuwa na lazima kwenda katika vyombo vya habari na kuishia ngazi ya familia,” amesema Makonda na kuongeza:
“Sikutaka kuongea na vyombo vya habari siyo kwa sababu sikutaka, ila sikujua niseme nini na mpaka leo nimefika hapa asubuhi sina cha kusema na zaidi nimemsihi Mungu anipatie neno la kusema mbele za watu juu ya mapenzi mema ya Ruge kwangu lakini bado hajanipa la kusema, naendelea kumuomba akinipa neno la kusema, akinipa kibali cha kusema atanipa na neno la kusema.”
Leave a comment