Anne Makinda, Spika mstaafu wa bunge la Tanzania, amesihi wanawake kusaidia wanawake wenzao kupata fursa walizotumia katika kufanikiwa maishani badala ya kufanya khiyana, anaandika Jasmin Seif.
Makinda amesema pale mwanamke anapokuwa amepanda kimadaraka anapaswa kusaidia wanawake wengine kufikia hatua aliyoifikia ili wanawake wengi zaidi wapate mafanikio.
Spika mstaafu Makinda ametoa nasaha hizo leo wakati akieleza uzoefu wake wa harakati za kupigania usawa wa mwanamke nchini.
Alikuwa mmoja wa watoa mada ya namna ya kufikia maendeleo ya mwanamke katika mhadhara ulioandaliwa na taasisi ya Kigoda cha Mwalimu Nyerere, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Amesema si desturi nzuri mwanamke kuiondoa ngazi iliyompandisha juu bali cha kufanya ni kumsaidia mwanamke mwingine kuitumia ngazi hiyo ili naye apate kupanga katika kutimiza ndoto yake ya kujikomboa kiuchumi.
Makinda amesema kwa hali inavyokwenda wanawake wanaelekea kuwa matajiri zaidi ya wanaume kwa sababu wanajitihada kubwa katika kufanya kazi.
Mbunge wa Hanang na waziri wa zamani wa utumishi, Dk. Mary Nagu yeye amesema si kweli kwamba wanawake hawapendani isipokuwa ukweli ni kuwa fursa kwao ni ndogo.
“Tunapendana sana sisi wanawake lakini kwa sababu fursa kwetu ni ndogo inakuwa kama mnapokuwa mnatumia mlango mdogo kupita, unamsukuma mwenzio ili upate nafasi ya kupita,” alisema.
Dk. Nagu alitamba kuwa wanawake wanauwezo mkubwa kuliko hata wanaume ila wanahaki ya kupewa nafasi kama wanazopata wanaume.
Anna Abdallah ambaye ni mwanasiasa mstaafu aliyefikia ngazi ya uwaziri, alisema ni muhimu sana wanawake kushirikiana kama wanataka kufanikiwa na kuondoka mfumo unaowarudisha nyuma kimaendeleo.
Amesema wakati akiwa kiongozi serikalini na katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) alikuwa akitetea wanawake kupata nafasi za uongozi, kazi aliyosema haikuwa rahisi.
“Wanaume walikuwa wakiuliza hivi hapa tumpeleke mwanamke kugombea, nilikuwa nashikilia kusema ndio ni haki yake, kwa sababu huo umalaya mnaosema si sifa ya mtu kupata uongozi.”
Tamasha la Kigoda cha Mwalimu lililo ana jana likikutanisha wasomi wa mataifa tofauti ndani ya Baraza la Afrika, linatarajiwa kumalizia kesho.
Leave a comment