MAKAMISHNA wanne wa Tume Huru ya Mipaka na Uchaguzi ya Kenya (IEBC), wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti, Juliana Cherera, wametaja sababu za kutokukubaliana na matokeo yaliyomtangaza William Ruto kuwa mshindi wa uchaguzi mkuu wa 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kenya … (endelea).
Wakizungumza katika hoteli ya Serena wanne hao wamedai mwenyekiti, Wafula Chebukati, alipingana nao na kusisitiza kutangaza matokeo licha ya wasiwasi wao.
Pia wamedai kuwa hesabu za mwisho ya matokeo ya uchaguzi wa urais haikuletwa mbele ya tume ili kushughulikiwa.
Wakiorodhesha sababu nne za uamuzi wao wa kukataa matokeo yaliyotangazwa, makamishna hao wamesema kuwa ujumlishaji wa matokeo haukuwa sahihi kimahesabu na kwamba matokeo hayo hayajumuishi jumla ya waliojiandikisha kupiga kura, kura zilizopigwa au zilizokataliwa.
Chebukati alimtangaza Ruto jana kuwa mshindi wa uchaguzi mkuu kwa kura 7,176,141 sawa na asilimia 50.49% mbele ya mshindani wake Raila Odinga wa Muungano wa Azimio la Umoja aliyepata kura 6,942,930.
Ruto pia alitangazwa kushinda katika kaunti 39 kwa asilimia zaidi ya 25 ya kura halali ikiwa ni zaidi yatakwa la kikatiba linalomtaka mshindi wa uarais kushinda angalau katika kaunti 25 kwa kupata angalau asilimia 25 ya kura halali.
Leave a comment