Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Makamba, Kinana watinga Ikulu
Habari za SiasaTangulizi

Makamba, Kinana watinga Ikulu

Spread the love

YUSUF Makamba na Abdulrahman Kinana, makatibu wakuu wastaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamebisha hodi kwa Rais John Magufuli. Anatipoti Mwandishi Wetu … (endelea).

Viongozi hao wakongwe, wamewandikia barua Dk. John Magufuli, Mwenyekiti wa CCM wakieleza kufedheheshwa na kudhalilishwa na Cyprian Musiba, mwanaharakati anayejitambulisha kuwa mtetezi wake (Rais Magufuli).

Barua hiyo ilianza kusambaa juzi tarehe 15 Julai 2019, ambapo wastaafu hao walieleza kushangazwa na ukimya wa taasisi za serikali dhidi ya Musiba ambaye wameeleza kuchafuliwa na kuzushiwa uongo.

Pius Msekwa, Katibu wa Baraza la Ushauri la Viongozi Wakuu Wastaafu wa CCM akizungumza na chombo kimoja cha habari nchini, licha ya kuthibitisha kupokea barua ya Makamba na Kinana, amesema (barua hiyo) pia imefikishwa kwa Dk. Magufuli na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa chama hicho.

Akizungumzia utaratibu wa kulikabili suala hilo, Msekwa amesema jambo hilo ndio linafikishwa kwa mara ya kwanza kwenye baraza hilo na kuwa, kitachofanyika ni kulifikisha kwenye chama ambacho ndio kina mamlaka ya kuitisha vikao.

“Ndio mara ya kwanza kupata malalamiko ya namna hii, tutafuata utararibu wa chama kuyashughulikia. Tunasuburi taratibu za chama tu,” amesema Msekwa.

Hata hivyo, Makamba jana alipoalikwa kwenye kipindi cha ‘Power Breakfast’ cha Clouds FM, alisema tamko lao halipaswi kuondolewa koma wala nukta, linatakiwa libaki kama lilivyo.

“Ni tamko refu, ni zuri, tumeliandika vizuri, tumeliandika mimi na rafiki yangu Kinana, halitakiwi kuongezwa kitu, libaki kama lilivyo,” alisema.

“Mara kadhaa ametutuhumu sisi wawili, makatibu wakuu wastaafu wa CCM kwa mambo ya uzushi na uongo,” walisema katika barua hiyo.

Hata hivyo, kwenye barua hiyo wamehoji Musiba “…anakingiwa kifua na nani? Tatu anatumika kwa malengo gani? Na nne nini hatima ya mikakati yote hii?

“Tafakari yetu inatupeleka kupata majibu yafuatayo; kwanza kwa ushahidi wa kimazingira mtu huyu anatumwa na kutumiwa na watu wenye uwezo wa kumlinda na kumkingia kifua bila kuhojiwa na taasisi yoyote wala mtu yeyote.

“Pili zipo ishara kwamba watu hawa wanaomkingia kifua wana mamlaka, baraka na kinga ambazo wamepewa ili kutekeleza majukumu maalumu kwa watu maalumu na kwa malengo maovu.

“Tatu: Mtu huyo anatumika kwa malengo ya kuwazushia, kuwakejeli, kuwavunjia heshima, kuwatia hofu na kuwanyamazisha viongozi, taasisi na watu ambao ni walengwa waliokusudiwa.

“Nne, kuna kila dalili kuwa lengo na hatima ya mkakati huu ni kuandaa tufani ya kuwahusisha walengwa, wastaafu na walio kazini katika nafasi mbalimbali na matendo ya kihalifu, kimaadili na kihaini ili kuhalalisha hayo wanayokusudia kuyafanya.

“Tumeamua kutochukua hatua za kisheria kwa sasa kwa sababu kwanza jambo hili lina taswira ya kimkakati na lina mtandao wenye malengo ya kisiasa. Kwa hiyo linapaswa kushughulikiwa kisiasa.

“Pili, unapochafuliwa, unachokwenda kudai mahakamani ni fidia. Kwetu sisi, heshima yetu haiwezi kuthaminishwa na fidia,” walisema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

error: Content is protected !!