MSIBA wa kada maarufu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro, Shambe Sagafu, umegeuka jukwaa la wanasiasa kukosoana huku wakitupiana vijembe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Kutokana na hali hiyo mwishoni mwa wiki, baadhi ya wana CCM walizitaka mamlaka husika ndani ya chama hicho, kuingilia kati malumbano hayo yanayodaiwa kuleta sintofahamu miongoni mwa wanachama wakiwamo viongozi wa CCM wa wilaya na mkoa.
Sintofahamu hiyo ilitokana na kauli anazodaiwa kuzitoa Mwenyekiti wa CCM Moshi Mjini, Alhaji Omar Shamba, alipopewa fursa ya kutoa salamu za rambirambi kwa niaba ya uongozi wa chama hicho.
Katika salamu zake, Alhaj Shamba alitoa kauli zilizoonekana kukosoa wana CCM waliokatwa majina, wakati wa mchakato wa kuwania nafasi ya kuipeperusha bendera ya CCM katika nafasi mbalimbali wakati wa uchaguzi mkuu mwaka juzi.
“Kuna waliokatwa majina, hadi leo hii pamoja na umri wao kuwataka wanisalimie niliowadizi umri, hawanisalimii na hata mimi napowasalimia hawaitiki salamu zangu,” alisema Alhaji Shamba.
Alisema tabia hiyo ni kinyume na maadili ya kidini, kwani hata kama kuna mtu alikatwa jina ni kutokana na taratibu za kichama na si utashi wa mtu binafsi.
Alhaji Shamba aliwataka watu kusameheana, jambo ambalo marehemu Shambe aliliishi, “wakati mimi nagombea nafasi niliyonayo sasa ya uenyekiti wa CCM wilaya ya Moshi, marehemu hakuwa upande wangu, jambo lililotufanya kukosana, pamoja na kwamba nilimlea kisiasa akiwa mdogo.
“Wakati nagombea uenyekiti wa CCM, Shambe hakuwa upande wangu, hakuniunga mkono kabisa, kiasi cha kwamba nilikwazika sana, lakini siku za hivi karibuni alinisimamisha njiani nikiwa kwenye gari, na dereva wangu ni shahidi.
“Aliniomba radhi kwa yaliyotokea na mimi nilimsamehe na huo ndio Uislamu unavyotaka,” alisema Alhaji Shamba.
Alhaji Shamba alisema uamuzi huo wa Shambe ni Uislamu na kwamba ndivyo Uislamu unavyotaka, akatoa ushauri kwa wenzake kufuata tabia hiyo.
Alisema Shambe ni tofauti na wengine waliokatwa majina, “na leo hii unapokutana nao hata hawakusalimii pamoja na umri wangu kutaka wanipe heshima hiyo.”
Katika kilichoonekana kumjibu Alhaji Shamba, mfanyabiashara mashuhuri wa mjini hapa, Alhaji Ibrahim Shayo ‘Ibra Line’ pamoja na kumwelezea marehemu Shambe kama mwanasiasa mzoefu aliyekipenda chama na kukitumikia ipasavyo, pia aliaka wazee ndani ya chama kujiheshimu na kuheshimu wengine.
“Marehemu Shambe nilichangia kwa kiasi kikubwa kushiriki kwake masuala ya chama na siasa na hata wakati mimi nagombea ubunge mwaka 2020, Shambe aliniunga mkono pamoja na kwamba nilishinda kwenye kura za maoni, lakini jina langu halikurudi, hatulaumu mtu, ni taratibu za chama changu,” alisema Alhaji Shayo.
“Naomba kutoa ushauri kwa wazee ndani ya CCM, kuheshimu wengine, wasipojiheshimu heshima wanayoitaka hawataipata, wapo wazee wanataka waheshimiwe, na wao basi wajenge tabia ya kujiheshimu na kuheshimu wengine, ndipo heshima wanayoitaka wataipata,” alisema Alhaji Shayo.
Leave a comment