MAJESHI ya nchi saba za Jumuiya ya Maendeleo ya Afrika (SADC), yameanza mazoezi ya kijeshi yenye lengo la kujiandaa na tishio la mashambulizi ya kigaidi na uharamia yanayoitikisa dunia, anaandika Mwandishi wetu.
Akizungumza katika uzinduzi wa mazoezi hayo yanayozishirikisha nchi saba zilizopo kwenye jumuiya hiyo, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi, wanajeshi wa nchi hizo watabadilishana uzoefu wa namna ya kukabiliana na vitendo vya kigaidi na uharamia.
Dk Mwinyi ameeleza kuwa mazoezi hayo yatawawezesha askari kupanua uzoefu katika masuala ya ulinzi na kuimarisha Umoja wa Maendeleo wa Nchi za Kusini (SADC).
“Tuna lengo la kujiweka tayari kwa misaada ya kijeshi katika kupambana na ugaidi na uharamia, baada ya hapo watapata uzoezfu mkubwa katika kukabiliana na vitendo hivyo vya kiharamia” amesema.
Ameeleza faida zitakazopatikana kutokana na mazoezi hayo kufanyika Tanga na nchini kwa ujumla ni pamoja na wananchi kupata tiba kipindi chote cha mwezi mzima pamoja na ujenzi wa miundombinu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Jenerali Venance Mabeyo amesema zaidi ya askari 600 kutoka nchi za Botswana, Lesotho, Zimbabwe, Afrika Kusini, Zambia, Malawi na Tanzania watashiriki katika mazoezi hayo yatakayodumu kwa mwezi mzima.
Leave a comment