MWANAMUME mmoja aliyefahamika kwa jina la Benard Mwendwa Musyoka (30), maarufu ‘Boy’ au ‘Swaleh’ amekutwa amefariki duniani katika chumba kulala wageni kwenye mtaa mmoja wa mabanda kaunti ya Nairobi nchini Kenya. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Kisanga hicho cha kutatanisha, kimethibitishwa na Mkuu wa polisi katika eneo la Makadara, Timon Odingo ambaye amefafanua kuwa tukio hilo limetokea katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Reli katika wadi ya Landi Mawe nchini humo.
Odingo aliongeza kwamba mwishoni mwa wiki Musyoka ambaye ni kondakta wa daladala maarufu kama ‘matatuu’ alifika katika Dreamland Guest House na kukodi chumba cha kulala.
“Mwanamume huyo alikodisha chumba alale kama mteja wa kawaida. Hata hivyo, kesho yake alikuwa mwili ukutwa kitandani huku akiwa tayari ameshafariki,” Odingo alisema.
Hata hivyo, familia ya marehemu inasema kifo cha ndugu yao kina hila na inataka polisi wachunguze zaidi.
Kwa mujibu wa mhudumu katika gesti hiyo ya Dreamland, Joel Mustapha, Musyoka enzi za uhai wake alikuwa mteja wa kila siku na hulala kati ya saa sita na saa saba za usiku.
Mustapha alivieleza vyombo vya habari nchini kuwa mteja wake alifika muda wa saa tatu usiku akilalamika ‘hasikii vizuri.’
Mustapha alisema kwamba hulipisha K Sh150 sawa na T sh 3,100 kwa kila chumba cha kulala.
“Aliniomba maji anywe dawa, pia aliniomba nimletee jaketi avae. Mimi namjua kama mtu ambaye husumbuliwa na kifafa na wakati mwingine huwa na matatizo ya kupumua,” Mustapha alisema.
Mustapha alieleza kwamba Musyoka alilala chumbani kwake na mwanamke mwingine anayefahamika kwa jina ‘Mwala’ ambaye pia ni mfanyabiashara wa parachichi mtaani hapo.
“Mwala aliamka asubuhi na kumwacha marehemu akiwa amelala. Hakusema ikiwa alikuwa amefariki au la wakati wa kutoka,” Mustapha alieleza.
Aidha, dadake marehemu, Beatrice Mwikali Musyoka (30), alipinga ripoti ya kifo cha kaka yake.
“Mwili wa kaka yangu ulikuwa na majeraha kifuani huku akiwa na damu mdomoni. Tunataka polisi wachunguze kisa hiki,” alisema Mwikali.
Mwenyekiti wa mtaa huo, Meritus Wanjala, alisema tukio hilo ni la tatu kutokea katika vyumba vya kulala wageni.
Leave a comment