WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameziagiza mamlaka husika kuchukua hatua kali za kisheria kwa watakaobainika kuwanyanyapaa na kuwabagua Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (WAVIU). Amesema vitendo, kauli au mitazamo ya unyanyapaa na ubaguzi kwa kundi hilo havikubaliki. Anaripoti Rhoda Kanuti … (endelea).
Ametoa agizo hilo leo tarehe 1 Desemba, 2021 katika Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika katika Uwanja wa Ruanda-Nzovwe mkoani Mbeya.
Majaliwa ambaye alikuwa akimuwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan amesema kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni “Zingatia Usawa. Tokomeza Ukimwi. Tokomeza Magonjwa ya Mlipuko.”
Majaliwa amesema nchi ina sheria ya UKIMWI ambayo imefanyiwa marekebisho kadhaa ili kuhakikisha kuwa huduma za VVU na UKIMWI zinamfikia kila mlengwa.
“Ninaelewa kuwa unyanyapaa na ubaguzi kwa WAVIU bado ni changamoto kubwa katika jamii zetu,” amesema.
Aidha, ameiagiza Wizara ya afya ianzishe uratibu wa kusikiliza na kutatua malalamiko, yatokanayo na unyanyapaa wa watu wanaoishi na VVU.
“Pili, ujenzi wa vituo vya vijana angalau kimoja katika kila kanda ili kuwajengea uwezo, ujuzi na stadi za maisha na kuwawezesha kiuchumi waathirika wa dawa za kulevya, washichana balehe na wanawake vijana.
“Tatu, muongozo wa unasihi usambazwe kwenye shule zote ili kuwezesha utoaji wa huduma hizo kwenye shule uweze kuzingatiwa,” amesema.
Ameiagiza Tume ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) ihakikishe mikakati ya kitaifa ya kisekta ya kudhibiti Ukimwi inazingatia na kukidhi takwa hili kwa kuzingatia mazingira ya nchi yetu.
Pia amesema sekta binafsi na umma zihamasishwe kuwekeza katika ujenzi wa viwanda kwa ajili ya vifaa, bidhaa za tiba, kwa zinazotibua ugonjwa wa Ukimwi katika nchi yetu ili tupunguze gharama za kuagiza kutoka nje.
“Sita, uwekezaji kwenye huduma ya kinga msingi
na kuyafikia makundi yaliyoko kwenye makundi hatari zaidi ya maambukizi mapya kama vile, wavuvi, madereva ya magari ya masa marefu, wachimbaji ili jamii isipate madhara,” amesema.
Leave a comment