WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema, hakuna anayekatazwa kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa ya kuambukiza. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Majaliwa ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, tarehe 20 Februari, katika Ibada ya kuuga mwili aliyekuwa katibu mkuu kiongozi, Balozi John Kijazi (64), iliyofanyika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Augustino, Korogwe jijini Tanga.
Maziko ya mwili wa Balozi Kijazi, aliyefariki tarehe 17yamefanyika nyumbani kwao, Korogwe jijini humo.
“Rais John Magufuli ametusihi kipindi chote, tuendelee kuzingatia masharti ya afya, nimeona hiyo tabia ambayo tulizungumza hata mwaka jana watu hawana tabia ya kunawa.”
“Lakini sasa wananawa, kutumia kitakasa mikono, barakoa utavaa pale ambapo unajua shughuli zako, zinahusihsa watu wengi, hakuna aliyekatazwa ni muhimu kila mmoja aende kwa tahadhari,” amesema Waziri Majaliwa.
Waziri Majaliwa amewashauri Watanzania kuwa makini na barakoa wanazotumia, hasa kwa kupendelea kutumia barakoa zinazotengenezwa nchini.
“Barakoa unazovaa wakati huo, tulisema ni bora kujiridhisha zinatoka, wapi bora ukatengeneza ya kwako au ukatumia iliyotengenezwa Tanzania. Ni jambo muhimu kulizingatia,” amesema Majaliwa.
Aidha, Majaliwa amewatoa hofu Watanzania akisema, Serikali inaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa ya kuambukiza, na kwamba wataalamu wa afya wanaendelea kuchunguza magonjwa hayo.
“Naomba kuwasihi Watanzania kwa wakati huu, dunia ikiwa kwenye mahangaiko ya magonjwa ya maambukizi, sisi tuwe watulivu serikali yenu inawapenda sana. Tumejikita katika kuhakikisha tunafuatilia na kuona mwenendo wa magonjwa haya,” amesema Waziri Majaliwa na kuongeza.
“Sisi tuna malaria, BP (shinikizo la damu), sukari, magonjwa chungu nzima, wataalamu wetu wako kwenye mahospitali, walio kwenye maabara wanaendelea na uchunguzi na kujikita katika kutoa huduma,” amesema
Tahadhari hiyo ya Waziri Majaliwa imekuja siku moja, tangu Rais Magufuli atangaze siku tatu za maombi zilizoanza jana Ijumaa hadi kesho Jumapili ya tarehe 21 Februari 2021.
Akizungumza katika ibada ya kuuaga mwili wa Balozi Kijazi iliyofanyika jana Ijumaa, katika Viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli aliwaomba Watanzani wazitumie siku hizo tatu kufunga, kusali na kuomba ili Mungu atokomeze tatizo la kupumua.
Kweli hakuna aliyekatazwa? Yule meya aliyewavua barakoa wananchi katika mkutano amechukuliwa hatua gani?
Pili, magonjwa mbali mbali yepi? Kwa nini mnashindwa kutamka kuwa Corona ipo?
Tatu, Kwani dawa zingine kutoka nje mbona hamzikatai? Ni barakoa tu ni mbaya?