Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Majaliwa azindua sherehe za uhuru, atoa maagizo mazito
Habari za SiasaTangulizi

Majaliwa azindua sherehe za uhuru, atoa maagizo mazito

Spread the love

 

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amezindua rasmi maadhimisho ya sherehe za uhuru wa miaka 60 Tanzania Bara na kuwataka Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya wimbi la nne la maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa korona (UVIKO- 19) ili virusi hivyo visiingie nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea)

Pia ametoa maagizo saba kwa kikosi kazi kinachoratibu ujenzi wa mji wa Serikali Dodoma, taasisi na wizara mbalimbali ili kuhakikisha taratibu za ujenzi na upangaji wa mji wa Dodoma zinazingatiwa.

Majaliwa ametoa maagizo hayo leo tarehe 2 Disemba, 2021 jijini Dodoma wakati akizindua wa maadhimisho ya sherehe za uhuru wa miaka 60 Tanzania bara pamoja na uzinduzi wa ujenzi wa miradi ya maendeleo katika mji wa Serikali Dodoma.

Uzinduzi wa miradi hiyo imejumuisha ujenzi wa maghorofa ya wizara 24 katika jiji hilo la Dodoma baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuidhinisha zaidi ya Sh bilioni 300 zitakazotumika katika ujenzi huo.

Amesema katika kuhakikisha azma ya kuwa mji wa kisasa inafikiwa kikamilifu, ujenzi wa mji wa kiserikali ufanyike kwa kuzingatia ramani na upangaji wa viwanja, zinazotokana na mpango kabambe wa mji wa serikali.

Amesema hali hiyo itasaidia kutokinzana na ujenzi wa miundombinu mingine inayotakiwa kujengwa kwenye eneo hilo na itakayojengwa hapo baadae juu na chini ya ardhi katika mji wetu wa serikali.

Ameagiza kikosi kazi kinachoratibu ujenzi huo wa mji wa kiserikali, kihakikishe wa majengo na ofisi za wizara unakwenda sambamba na ujenzi wa miundombinu mingine mingine kama vile umeme, maji safi na maji taka, mawasiliano na usalama wa zimamoto na uokoaji.

“Ofisi ya waziri mkuu kwa kushirikiana na wizara ya viwanda na biashara endeleeni kuwasiliana na wazalishaji wa ndani wa bidhaa za ujenzi, ikiwemo saruji, nondo, mchanga, kokoto, ili utaratibu wa manunuzi mapema ina kuwezesha uzalishaji wa vifaa vya kutosha vyenye ubora unaohitajika.

“Hali hii iende sambamba wizara ya viwanda na biashara kuhimiza viwanda vyetu kuzalisha bidhaa hizi kwa wingi na hakuna sababu ya kupandisha gharama eti kwa sababu serikali sasa inajenga majengo 24 hiyo haitakubalika,” amesema.

Pia ameagiza kikosi kazi hicho, kushirikiana na wizara zote, kuainisha mahitaji ya fedha katika mwaka ujao wa fedha wa 2022/2023, ili yatengewe fedha katika kipindi husika majengo yakamilike kwa wakati.

Aidha, Kamati maalumu ya makatibu wakuu wanaosimamia ujenzi huo, nao wameagizwa kuhakikisha kwamba ujenzi unatekelezwa kwa mujibu wa mpango kazi iwe ndani ya bajeti, muda, ubora na usalama.

“Wizara ya fedha na mipango ihakikishe fedha zinazohitaji katika ujenzi huu zinapatikana kwa wakati ili ujenzi uende bila kukwama.

“Mwisho, kikosi kazi hiki kishirikiane na taasisi husika kikamilishe maandalizi ya ujenzi wa huduma mbalimbali za kijamii katika mji huu kama vile viwanja vya michezo, vituo vya bodaboda na nyumba za ibada.

Aidha, akizungumzia kuhusu maadhimisho hayo ya sherehe za uhuru wa Tanzania bara, Majaliwa amesema kilele chake ambacho kitafikiwa tarehe 9 Disemba mwaka huu, mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Amesema sherehe hizo za uhuru zitafanyika siku mbili kabla katika mikoa mingini ili kutoa fursa kwa wananchi kufuatilia hotuba za viongozi katika siku hiyo ya tarehe tisa.

Awali Katibu wa Kikosi Kazi cha Kuratibu Serikali kuhamia Dodoma Meshack Bandawe amesema Wakala wa majengo – TBA wamejipanga kuanza ujenzi wa nyumba 100 za viongozi katika mji wa serikali.

“Wizara ujenzi na uchukuzi katika mwaka wa fedha, 2020/2021 wametenga Sh bilioni 9.1 ili kuiwezesha TBA kuwa fedha za kuanzia ujenzi huu.

“Ujenzi utaanza baada ya kukamilisha ulipaji wa fidia katika eneo lililopo kati ya eneo la serikali na Ikulu ya Chamwino lenye ukubwa hekari 2030.88,” amesema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Chadema yamtaka Rais Samia aunde tume kuchunguza mauaji mgodi wa Barick

Spread the loveRAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameombwa aunde tume huru kwa...

KimataifaTangulizi

Zuma akataliwa kugombea urais

Spread the love  TUME Huru ya Uchaguzi Afrika Kusini (IEC) imemwondoa rais...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

error: Content is protected !!