WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameunda timu maalum ya watu tisa ambayo imepewa jukumu la kuchunguza mauaji yaliyofanyika Mtwara na Kilindi, mkoani Tanga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
“Kamati hiyo inapaswa kuanza kazi yake kesho na inatakiwa iwe imekamilisha ripoti yake ndani ya siku 14,” amesema Waziri Mkuu ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa leo Ijumaa, tarehe 4 Februari 2022 mjini Magu, Mwanza akiwa njiani kuelekea Musoma, Mara kwenye maadhimisho ya miaka 45 ya CCM.
Rais Samia amesema anatambua Jeshi la Polisi limeunda kamati ya uchunguzi lakini ameagiza iundwe kamati hiyo huru ili ikafanye uchunguzi wa mauaji ya Mtwara yaliyofanywa na askari polisi.
Mauaji ya Mtwara yalitokea 5 Januari 2022 na mauaji ya Kilindi yaliyotokea 30 Januari 2022.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, Kamati hiyo ina maafisa wenye dhamana kutoka mamlaka tofauti za Serikali ikiwemo Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Rais, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Ofisi ya Mwanansheria Mkuu na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amemuagiza Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro awasimamishe kazi maafisa wa Polisi wa Mtwara na Kilindi ili kupisha uchunguzi wakati timu aliyoiunda ikifanya kazi yake.
“Viongozi hawa wanapaswa wakae pembeni, watahojiwa na hii timu wakiwa nje ya ofisi,” amesema Waziri Mkuu na kuwataja maafisa hao kuwa ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara (RPC), Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Mtwara (RCO) na Mkuu wa Kituo cha Polisi Mtwara cha eneo alilofia mfanyabiashara Mussa Hamisi Hamisi na Mrakibu Msaidizi wa Polisi Greyson Mahenge anayedaiwa kujinyonga akiwa mahabusu.
Aidha, Waziri Mkuu ameagiza Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Kilindi na Afisa Upelelezi wa Wilaya nao pia wakae pembeni kupisha uchunguzi.
Leave a comment