WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameitaka Kampuni ya Kimataifa ya Kuhudumia Makontena Tanzania (TICTS) kuimarisha utendaji kazi wake ikiwemo kuacha kuchelewesha ushushaji wa mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Amesema kampuni hiyo ina paswa kufanya kazi kwa weledi na kupitia mkataba wa utendaji kazi wake ili kuhakikisha inatoa huduma stahili kwa wateja wanaohudumiwa na bandari hiyo na kuwa kimbilio.
Ametoa agizo hilo leo Ijumaa, tarehe 8 Aprili 2022, jijiji Dar es Salaam wakati alipozungumza na Viongozi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na TICTS kisha kukagua utendaji kazi wa Bandari ya Dar es Salaam kufuatia maagizo ya Rais Samia Suluhu Hassan.
“Tunataka mrejesho mzuri kutoka kwa wateja wetu, bandari hii ndio injini ya uchumi wetu, hatutasita kufanya mapitio ya mkataba wa TICTS, wapo wawekezaji wengi ambao wana nia ya kuwekeza kwenye eneo hilo, hatuwezi kuvumilia kuona kuna ucheleweshwaji wa utoaji wa mizigo bandarini,” amesema
Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa amesema wizara itaendelea kuisimamia TPA ili kuhakikisha wanaendelea kupunguza zaidi na kwa wakati shehena yote inayopita kwenye bandari hiyo.
“Bandari ni sehemu muhimu kwenye uchumi wetu, tutahakikisha maeneo yote ambayo hayatumiki kuhifadhi mizigo yanaanza kutumika ili kuondoa msongamano,” amesema
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Eric Hamisi amesema wameendelea kufanya maboresho katika bandari hiyo ili kuongeza ufanisi ikiwemo kununua vifaa vipya kama vile Reach Stracker Saba (7) na FolkLift mbili (2) za tani 16 kila moja.
Leave a comment