WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Lindi, Pudencis Protas kumkamata Kaimu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) wilaya ya Ruangwa Anthon Mandai kutokana na tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo Jumapili, Agosti 12, 2018, wakati akizungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Ruangwa akiwa katika siku ya mwisho ya ziara kyake ya kikazi wilayani hapa. Mandai anakaimu nafasi hiyo tangu Juni, 2012.
Ametoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa walimu wakimlalamikia kiongozi huyo kuwa na tabia za kudai rushwa, kutowapandisha madaraja, ulevi pamoja na kuwaita walimu hao kwenye vilabu vya pombe kwa ajili ya kuwasikiliza matatizo yao.
Amesema mbali na kulalamikiwa na walimu kwa tuhuma mbalimbali zikiwemo za ulevi na kuwaita walimu katika vilabu vya pombe pindi wanapohitaji kuhudumiwa, pia amekuwa akighushi nyaraka za mirathi, jambo linalosababisha baadhi ya familia za waliokuwa walimu kuchelewa kupata haki zao.
“Huyu Katibu ameshindwa kuwasaidia walimu katika kutatua changamoto zao na badala yake amekuwa akitumia vibaya majina ya viongozi wakuu, ambapo hata mimi alijaribu kutaka kunichakachua kwa kughushi muhtasari wa kikao cha mirathi ya Mwalimu Suwedi Chikawe akitumia jina langu kuwa nilikuwa mwenyekiti wa kikao hicho kilichokuwa na agenda ya kumbadilisha msimamizi wa mirathi aliyeteuliwa na familia jambo ambalo si la kweli,” amesema.
Waziri Mkuu amesema mbali na kukamatwa kwa Bw. Mandai, pia amemuagiza Kamanda Pudencis afanye uchunguzi wa kina utakaowezesha kukamatwa kwa mtandao wa watu wote wanashirikiana na kiongozi huyo katika kughushi nyaraka za vikao vya mirathi.
Leave a comment