WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, ameshauri aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati John Magufuli, aenziwe kwa kutimiza ndoto yake ya uanzishwaji somo la histori ya Tanzania, shuleni. Anaripoti Matilda Peter, Dar es Salaam … (endelea).
Majaliwa ametoa wito huo leo Ijumaa, tarehe 21 Mei 2021, katika Kongamano la kutambua na kuuenzi mchango wa Tanzania kwenye ukombozi wa Bara la Afrika, lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa, cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika kongamano hilo, Majaliwa amewashauri washriki wake pamoja na Watanzania, kuhakikisha ndoto hiyo ya Dk. Magufuli, inatimizwa kwa somo hilo kufundishwa kwenye ngazi zote za elimu.
Dk. Magufuli aliyefariki dunia akiwa madarakani, tarehe 17 Machi 2021, alitoa agizo hilo tarehe 9 Desemba 2020, akiwaapisha mawaziri Ikulu jijini Dodoma.
Katika maagizo hayo, Dk. Magufuli aliiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, ianzishe mtaala wa somo hilo, huku akisisitiza liwe la lazima kufundishwa shuleni.
Dk. Magufuli alisema somo hilo litasaidia kuwajengea uzalendo Watanzania, hasa vijana waliozaliwa baada ya uhuru.
Hadi anafariki dunia, Wizara ya Elimu ya Elimu ilikuwa imeshakamilisha mihutasari ya vitabu vya somo hilo na kuahidi litaanza kufundishwa shuleni Julai 2021.
Mwanasiasa huyo aliyefariki dunia katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, mwili wake ulizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, tarehe 26 Machi 2021.
Leave a comment