WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Watanzania waendelee kuliombea Taifa lidumu katika hali ya amani na utulivu, anaandika Dany Tibason.
Majaliwa amesema suala la kudumisha amani na utulivu ni jukumu la kila mmoja, hivyo kila mwananchi kwa imani yake ahakikishe anashiriki kutunza hali hiyo.
Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya kumalizika kwa kuswali sala ya Ijumaa katika Msikiti wa Al-Gadaf, mjini Dodoma.
“Ni vyema kila mwananchi akajivunia hali ya amani na utulivu iliyoko nchini kwa kuwa ndiyo inayowezesha kufanyika kwa shughuli mbalimbali za kimaendeleo,” amesema.
Pia amewataka wazazi wahakikishe wanawalea watoto wao katika mazingira ya kidini ili wanapokuwa watu wazima wawe raia wema wenye kuwa na uzalendo na nchi yao.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewakumbusha Waislamu wahakikishe wanautumia vizuri mwezi mtukufu wa Ramadhan kwa kuzidisha ibada na kusaidia watu wenye mahitaji.
Ibada hiyo ya sala ya Ijumaa iliongozwa na Sheikh Nurdin Kishki ambaye ni Imamu wa Msikiti wa Vetenari, wilayani Temeke, jijini Dar es Salaam.
Sheikh Kishki katika hotuba yake, amewasisitiza Waislamu waendelee kufanya mambo mema yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu ikiwemo kuwatunza wazazi wao, kumswalia Mtume Mohammed (S.A.W) na kufunga katika mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Awali sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Shabani Rajabu kabla ya Kuwakaribisha Waziri Mkuu na Sheikh Nurdin Kishki aliwataka waumini wa Dini ya Kiislamu kwa watu wenye upendo kwa kila mtu.
Rajabu amesema kwa mafundisho ya Mtume Mohamad (S.A.W) amehimiza upendo kwa watu wote ikiwa ni pamoja na kwakarimu wale wote ambao wanauhitaji wa kimwili na kiroho.