WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amejikuta akibubujikwa machozi, mbele ya jeneza lenye mwili wa aliyekuwa Rais wa Taifa hilo, Dk. John Pombe Magufuli. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Majaliwa akiwa ameongozana na mkewe, Mary mara baada ya kufika mbele ya mwili wa Dk. Magufuli, Majaliwa alisimama kutoa heshima za mwisho, kasha akatoa kitambaa chake na kuanza kujifuta machozi.
Mara baada ya kumaliza kutoa heshima za mwisho, Majaliwa aliondoka.
Shughuli ya kuaga imeongozwa na Rais wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan.
Baadhi ya viongozi wengine waliotoa heshima za mwisho ni; Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Bashiru Ally, Spika Mstaafu Anne Makinda, Rais mstaafu wa Zanzibar, Aman Abeid Karume na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Hemed Sulieman Abdulla.
Pia, Mama Maria Nyerere, Mjane wa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Wengine ni, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika na Naibu wake upande wa Zanzibar, Salum Mwalimu, mawaziri na naibu mawaziri, katibu wakuu na naibu wao, wakuu wa mikoa na wilaya, wakuu wa taasisi mbalimbali za serikali na siasa.
Mwili wa Hayati Magufuli utaagwa rajiwa kuagwa Dar es Salaam kwa siku mbili (Jumamosi na Jumapili), kisha tarehe 22 Machi 2021, mwili huo utaagwa katika Makao Makuu ya Nchi Dodoma.
Tarehe 23 Machi 2021, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa visiwani Zanzibar, kisha utasafirishwa Mwanza kwa ajili ya shughuli ya kuuaga tarehe 24 Machi 2021.
Baada ya kuagwa Mwanza, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa na wananchi wa Chato mkoani Geita, tarehe 25 Machi mwaka huu.
Pumzika kwa Amani, Al Marhoum. Utakumbukwa Daima – RIP