WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema, Serikali imepokea na itayafanyia kazi malalamiko ya wabunge juu ya utaratibu wa ukaguzi unaofanywa kwenye mgodi wa Mererani, mkoani Arusha. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Majaliwa alitoa kauli hiyo jana Alhamisi, tarehe 29 Aprili, 2021, wakati akijibu hoja ya Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka ambaye alitaka maelezo juu ya utaratibu wa ukaguzi katika mgodi huo.
Mbunge huyo alikuwa akichangia mjadala wa hotuba makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini.
Mwingine alikuwa ni mbunge wa Geita, Joseph Msukuma aliyesema, ukaguzi umekuwa ukifanyika kwa kuvuliwa nguo, jambo ambalo ni kinyume na utaratibu na unakiuka utu wa mwanadamu.
Majaliwa alisema “nimesikia concern ya namna ukaguzi, unavyoendelea katika mgodi wa Mirerani, nilipanga kutembelea Mirerani ili kuona hali hiyo na kutafuta ufumbuzi, nikuahidi Mhe. Spika na waheshimiwa wabunge, tumepokea na Serikali tutalifanyia kazi.”
Alisema Serikali inapata fedha nyingi kupitia madini ya Tanzanite yanayochimbwa katika mgodi huo hivyo haiwezi kushindwa kununua mtambo unaoweza kufanya ukaguzi wenyewe bila kusumbua mtu.
Leave a comment