MAJAJI wa Mahakama Kuu Zanzibar na mahakimu visiwani humo, wameombwa kuwa mstari wa mbele katika kudhibiti vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu, kupitia nafasi zao kwenye mhimili huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Wito huo umetolewa katika semina ya siku mbili, tarehe 27 na 28 Novemba 2021, ya kuwakumbusha namna ya kushughulika na mashauri ya haki za binadamu, iliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC).
Kaimu Jaji Mkuu Zanzibar, Hamis Ramadhan, amewataka majaji na mahakimu kushughulikia kwa wakati kesi za udhalilishaji wanawake na watoto, ili kutokomea vitendo hivyo.
“Kumekuwa na ongezeko kubwa la kesi za udhalilishaji wanawake na watoto hapa Zanzibar, mafunzo haya yatusaidie kuona umuhimu wa kushughulikia mambo haya,” amesema Jaji Ramadhan.
Naye Kamishna kutoka Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) Zanzibar, Khatib Mwinyi Chande, amesema mahakama ni taasisi inayopaswa kuisaidia Serikali kutatua matatizo ya wananchi wake.
“Kufungua mashauri mahakamani ni namna pekee ya kutetea na kukomesha uvunjaji wa aina yoyote wa haki za binadamu ambazo ni za muhimu kwa kila mtu. Mahakama ni taasisi zinazopaswa kuisaidia Serikali kutatua matatizo hayo na si vinginevyo,” amesema Chande.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa amesema mtandao huo umeandaa mafunzo hayo kwa majaji na mahakimu, ili kuwakumbusha umuhimu wao katika mashauri yanayohusiana na haki za binadamu.
“Tunatambua kuwa majaji na mahakimu ni watetezi muhimu wa haki za binadamu, tuitaendelea kuwa na utaratibu huu wa mafunzo ili kukumbushana wajibu wetu,” amesema Olengurumwa.
Leave a comment