MAHAKAMA ya Tanzania imebadili mfumo wake wa uendeshaji, na sasa wamejielekeza kutumia teknolojia zaidi katika utoaji wa haki. Anaripoti Faki Sosi …(endelea).
Leo tehere 29 Julai mwaka 2019, mahakama imesaini mkataba wa Sh 4.2 bilioni na Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), kwa ajili ya kuweka mtandao mpana (WAN), kwenye mahakama zote nchini utakaosaidia kupunguza mrundikano wa kesi.
Kelege Enock, Mkurugenzi wa Tehama wa Mahakama ya Tanzania wakati utiaji wa saini hiyo amesema, teknolojia hiyo isaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli na kusaidia shahidi kuwasilisha ushahidi wake bila kulazimika kufika mahakamani.
Amesema, huduma hiyo pia itawasaidia mawakili au wananchi kufungua shitaka au shauri kwa njia ya mtandao bila kulazimika kufika mahakamani.
Kelege ameeleza, mahakama imeingia mkataba huo na TTCL kwa ajili ya kuunganisha majengo ya mahakama kuanzia Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na baadhi ya Mahakama za Mwanzo zenye majengo ya kisasa.
Amesema, jitihada hizo hazijaanza leon tangu mwaka 2015 na kwamba wamefanikiwa kusaini mkataba wa Sh.4.2 bilioni.
“Mahakama zitakazo ingizwa kwenye mtandao ni pamoja na Mahakama ya Rufani moja, Mahakama Kuu 16, Mahakama Kuu Maalumu (Specialized Divisions) nne, Mahakama za Mkoa 29, Mahakama za Wilaya 112, Mahakama za Mwanzo 10 hivyo kufanya jumla ya majengo ya Mahakama 157 kwa kuanzia,” amesema.
“Kwa kuzingatia unyeti na usalama wa shughuli za Mahakama huduma hii ya mtandao itawezeshwa na teknolojia ya “Virtual Private Network (VPN)” kupitia ‘‘Multiprotocol Labelling Switch (MPLS)’’. amesema
Alisema faidi nyingine ya mtandao huo ni kuwepo kwa mazingira wezeshi ya kubadilishana taarifa kati ya Mahakama na Taasisi wadau katika Mfumo mzima wa utoaji Haki nchini.
“Taasisi wadau ni pamoja na Magereza, Polisi, Ofisi ya Mwendesha Mashitaka, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Chama Cha Mawakili (TLS),” amesema.
Waziri Kindamba, Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, ameeleza kuwa shirika hilo limekuwa likiuza data katika kampuni zingine za mawasiliano kutokana na hilo wanawahakikishia mahakama kuwa wataifanya kazi hiyo na kuimaliza kwa wakati.
“Tunajivunia kuwa sehemu ya watu watakaowasaidia watanzania kupata haki kwa haraka hivyo tunaishukuru mahakama kwa kutuchagua kwani kutokana na miradi hii ndio inayowezesha kuwepo kwa gawio linalorudi serikalini,” amesema.
Leave a comment