MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, imewahukumu kifo, watu watano waliopatikana na hatia ya kumuuwa kwa makusudi, Dk. Sengodo Mvungi, aliyekuwa mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Akisoma uamuzi huo, leo Ijumaa, tarehe 18 Septemba 2020, Jaji wa mahakama hiyo, Kulita Seif Kulita amesema, amefikia maamuzi hayo, baada ya kujiridhisha na ushahidi uliotolewa mbele ya mahakama yake.
Maamuzi haya yanatolewa, takribani miaka 7 tokea mwanasheria huyo nguli na mwanaharakati wa kutetea katiba, alipovamiwa na kuawa, nyumbani kwake, jijini Dar es Salaam.
Dk. Mvungi ambaye alikuwa pia Mhadhiri Mwandamzi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Bagamayo (UB), alivamiwa usiku wa kuamkia tarehe 3 Novemba 2013 na kukatwa kwa mapanga maeneo mbalimbali mwilini, ikiwemo sehemu za kichwani kwa madai ya kutaka awapatie fedha.
Taarifa zinasema, wauwaji wa Dk. Mvungi, kabla ya kuvunja milango ya nyumba yake, walilipua kitu ambacho kilitoa moshi mwingi na cheche kisha kuingia ndani na kuanza kudai wapewe fedha.
Dk. Mvungi, alikuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC), kupitia chama cha NCCR- Mageuzi;
katika tukio hilo, Dk. Mvungi alijeruhiwa vibaya hasa kichwani na alikuwa amepoteza fahamu kabisa hata aliposafirishwa na kupelekwa nchini Afrika Kusini kwa matibabu zaidi.
Kabla ya kuanza kujitetea, washitakiwa hao, walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, tarehe 22 Novemba 2013, kusomewa mashitaka yaliyokuwa yakiwakabili.
muua Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Dk.Sengondo Mvungi baada ya kutiwa hatiani.
Aidha, Mahakama Kuu imemuachia huru mshtakiwa Juma Kanungu, baada ya upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha mashtaka pasipo kuacha mashaka dhidi yake.
Waliohukumiwa kifo, ni Msigwa Matonya, Mianda Mlelwa, maarufu kama white, Paul Mdonondo, Longishu Losingo na John Mayunga maarufu kama Ngosha.
Akisoma hukumu hiyo, Jaji Kulita amesema, upande wa mashtaka kupitia mashahidi 16 waliofika mahakamani hapo kutoa ushahidi na vielelezo 15 wameweza kuthibitisha pasipo na shaka kuwa watuhumiwa hao watano wametenda kosa hilo la mauaji.
Amesema, “…ushahidi na vielelezo vilivyotolewa na upande wa mashtaka vimeweza kuthibitisha bila kuacha shaka yoyote, kwamba wahusika wametenda kosa.”
Ameongeza, “hivyo mahakama inawahukumu washtakiwa watano kati ya sita, kunyongwa mpaka kufa.”
Jaji Kulita amesema, Kanungu ameachiwa huru baada ya ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka, kutomgusa kwa kiwango ambacho hakina shaka.”
Leave a comment