MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Arusha, imewaacha huru viongozi na wanachi 24 wa Wilaya ya Ngorongoro, waliokuwa wanakabiliwa na kesi ya kupanga njama za mauaji ya Askari Polisi, baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kuwasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea nayo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Viongozi hao wameachwa huru leo Jumanne, tarehe 22 Novemba 2022, na mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi, Herieth Mhenga, wakati kesi iliyokuwa inawakabili Na. 11/2022 ilipokwenda kwa ajili ya kutajwa.
Kesi hiyo ya mauaji imefutwa baada ya Mawakili wa Jamhuri kuieleza mahakama hiyo kuwa, DPP hana nia ya kuendelea nayo na kuomba washtakiwa wake waachwe huru chini ya kifungu Cha 91 Cha Sheria ya Mwenendo wa Jinai nchini.
Viongozi na wanachama hao wameachwa huru baada ya kusota rumande takribani miezi mitano, tangu walipokamatwa katika nyakati tofauti kuanzia Juni Hadi Julai 2022.
Uamuzi huo wa DPP umekuja ikiwa zimepita siku kadhaa tangu mahakama hiyo kuitaka Jamhuri kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo baada ya mara kadhaa kudai haujakamilika.
Kesi hiyo ilikuwa na washtakiwa 24, akiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wilayani Ngorongoro, Ndirango Olesenge Laizer; Diwani wa Kata ya Piyaya, Simon Orosokiria; Diwani viti maalum, Kijoolu Kakeya.
Wengine ni Diwani wa Ololosokwani, Moloimet Yohana; Diwani wa Malambo, Joel Lessonu; Diwani viti maalum, Talengo Leshoko; Diwani wa Oloirien, Shengena Killel; Diwani wa Arash, Mathew Eliakimu na Diwani wa Maaloni, Damiani Laiza.
Washtakiwa hao waliwekwa kizuzini tangu tarehe 16 Juni 2022, wakikabiliwa na mashtaka mawili, la kwanza wanatuhumiwa kupanga njama ya kuwa maofisa wa Serikali na polisi, watakaoshiriki zoezi la kuweka mipaka katika pori tengefu la Loliondo.
Shtaka la pili ni la mauaji ya askari polisi mwenye namba G 4200, Koplo Garlus Mwita, wanalodaiwa kulitenda tarehe 10 Juni mwaka huu, maeneo ya Ololosokwan, wilayani Ngorongoro.
Leave a comment