Mahakama ya Katiba nchini Uganda imefuta sheria iliyokuwa imepiga marufuku wanawake na wasichana nchini humo kuvaa nguo fupi kufuatia shinikizo la wanaharakati. Imeandaliwa na Gabriel Mushi, Dar es Salaam … (endelea).
Sheria hiyo ambayo ilipitishwa mwaka 2014, pia ilikuwa inanuia kuzuia usambazaji wa picha za ngono mtandaoni ili kuwalinda wanawake na watoto.
Hata hivyo, waliopinga sheria hiyo walihoji kuwa kanuni hiyo ilitumiwa vibaya na kusababisha wanawake waliovaa nguo fupi kushambuliwa mtaani.
Wakitoa uamuzi wao jana tarehe 18 Agosti, jopo la majaji watano wa Mahakama hiyo kwa kauli moja waliamua kuwa vifungu vya sheria hiyo vinakiuka katiba.
Majaji hao walisema hakutakuwa na madhara yoyote kwa wanawake na wasichana kuvalia mavazi yanayoonyesha maungo yao.
Baada ya sheria hiyo maarufu ‘sheria ya minisketi’ kupitishwa, kulikuwa na maandamano makubwa jijini Kampala kupinga wanawake kufanyiwa ukatili mitaani pindi walipovaa nguo fupi.
Wanaharakati wa kutetea haki za binadamu walikwenda mahakamani wakitaka sheria hiyo ifutwe na sasa imetupiliwa mbali.
Leave a comment