MAHAKAMA ya Wilaya ya Ngorongoro, Mkoa wa Arusha Arusha, imezifuta kesi tisa za kuishi nchini kinyume cha sheria zilizokuwa zinawakabili wakazi 62 wa Kata ya Loliondo mkoani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Kesi hizo zilizofunguliwa kati ya Juni na Julai, 2022 zimefutwa jana tarehe 17 Novemba mwaka huu, chini ya kifungu cha 225 (5) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuleta mashahidi ili kuthibitisha mashtaka yao bila kuacha shaka yeyote.
Akizungumza na MwanaHALISI Online kwa simu, leo Ijumaa, tarehe 18 Novemba 2022, Paul Kisabo, akitokea Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), ambao walikuwa wanasimamia kesi hizo, amesema mahakama hiyo imefuta kesi hizo na washtakiwa wako huru.
“Kesi hizo zilikuwa zinawahusu watu waliokamatwa na kushtakiwa kwa kuishi nchini kinyume cha sheria. Jana kesi hizo zimefutwa, mahakama iliamua kuzifuta sababu upande wa Jamhuri wameshindwa kuleta mashahidi kwa ajili ya kuthibitisha mashtaka yao dhidi ya watu hao,” amesema Wakili Kisabo.
Miongoni mwa kesi zilizofutwa ni kesi ya jinai Na.17/2022, iliyokuwa inawakabili wawili, ambapo mshtakiwa wa kwanza ni Raia wa Kenya, Rebeka Koriata, aliyeshtakiwa kwa kosa la kuishi na kufanya kazi nchini kinyume cha sheria katika Kijiji cha Olorosokwani wilayani Ngorongoro bila ya hati ya kusafiria na kibali cha kuishi nchini.
Mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, ni Mtanzania Jacob Koriata, aliyeshtakiwa kwa kumhifadhi kinyume cha sheria mshtakiwa wa kwanza, Rebeka, ambaye ni Raia wa Kenya, ambapo aliishi naye kama mke tangu 2006 huku akijua kuwa ni raia wa kigeni asiyekuwa na hati ya kusafiria wala kibali kinachomruhu kuishi Tanzania.
Kesi nyingine ni Na. 8/2022, iliyokuwa inawakabili Raia saba wa Kenya, wakiongozwa na Sanare Salonik, walioshtakiwa kwa kuishi kwenye Kijiji cha Njorooi wilayani Ngorongoro, bila ya hati ya kusafiria na kibali cha kuishi nchini.
Wakazi hao wa Loliondo walikamatwa kati ya Juni na Julai mwaka huu, wakati wa zoezi la uwekaji mipaka katika eneo la kilomita 1,500 , lililoendeshwa na Serikali.
Leave a comment