MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kivukoni/Kinondoni imetoa amri ya kufukuliwa mwili wa Stella Moses ili ufanyiwe uchunguzi kujua chanzo cha kifo chake baada ya kupoteza maisha katika mazingira ya kutatanisha akiwa mahabusu kwenye Kituo cha Polisi cha Mburahati, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Uamuzi huo umetolewa leo Jumatatu, tarehe 19 Desemba 2022 na Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Franco Kiswaga akitoa uamuzi wa maombi yaliyowasilishwa na shemeji yake marehemu, Emmanuel Kagongo, kuomba itoe amri Kwa mamlaka husika kuchunguza kifo cha Stella.
Ni katika shauri dogo la jinai Na. 3/2022, lililofunguliwa mahakamani hapo Machi 2022, dhidi ya Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) na wenzake watano ikiwemo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), ikiwa imepita zaidi ya mwaka mmoja tangu Stella afariki Dunia tarege 20 Desemba 2020.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Kiswaga amesema mahakama imetoa amri hiyo chini ya Sheria inayosimamia vifo vyenye mashaka Sura ya 24 ya Sheria za Tanzania, baada ya kukosekana ripoti ya uchunguzi dhidi ya kifo hicho.
“Hata katika viapo kinzani hakuna ripoti yeyote ya polisi au mkemia mkuu wa Serikali kwamba alichukuliwa sampuli kuelekea kwa mkemia mkuu na hakuna taarifa iliyotolewa kuhusu uchunguzi huo kama umefanyika lakini mahakama haijapata taarifa ya uchunguzi kuhusiana na chanzo cha kifo cha marehemu,” amesema Jaji Kiswaga na kuongeza:
“Hivyo basi, mahakama inaona maombi ya mleta maombi yana mashiko na hivyo basi mahakama hii inaamuru kufanyike uchunguzi katika mwili wa marehemu Stella Moses ambaye kulingana na mleta maombi, mahakama imetambua amekufa kifo kisicho cha kawaida katika ofisi ya umma. Uchunguzi ufanyike taarifa itolewe mahakamani yeyote atakayehusika na kifo hicho achukuliwe hatua kwa mujibu wa Sheria.”
Emmanuel kupitia Wakili Peter Mdeleka, aliwasilisha maombi hayo akiiomba mahakama itoe amri ili mwili wa Stella ufukuliwe kwa ajili ya kufanyiwe uchunguzi, akidai kwamba Hospitali ya Muhimbili haikueleza chanzo cha kifo chake badala yake ilisema uchunguzi unaendelea.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi lilitoa taarifa iliyodai kwamba Stella alifariki Dunia Kwa kujinyonga akiwa ndani ya kituo Cha polisi.
Mwili wa Stella ulizikwa Goba jijini Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya uamuzi huo, Wakili Madeleka, alisema wanaandika barua kwa mahakama hiyo Ili kupata nakala ya uamuzi kwa ajili ya taratibu zinazofuata.
Wakili Madeleka alidai kuwa, uamuzi huo ni ujumbe tosha kwa vyombo vya dola kuheshimu haki za mahabusu wakiwa kizuizini.
Wakili huyo amedai kuwa, baada ya taratibu za kisheria kukamilika, atatoa taarifa kwa umma juu ya kinachoendelea kuhusu uchunguzi huo, kama marehemu aliuawa au alikufa kifo cha asili.
Alisema kuwa, kama itabainika aliuawa, Sheria zitafuata mkondo wake kwa mhusika.
Leave a comment