MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, imefuta uamuzi wa Kamati ya Maadili ya Mawakili Tanganyika, wa kumfuta uwakili, Mwanaharakati Fatma Karume. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kamati hiyo ilimvua uwakili Fatma na kuondoa namba yake ya uwakili ( 848), katika orodha ya mawakili wa Tanganyika, tarehe 23 Oktoba 2020, kwa tuhuma za kukiuka maadili ya taaluma hiyo, katika kesi ya kupinga uteuzi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Prof. Adelardius Kilangi.
Kwa mujibu wa Wakili wa Fatma Karume, katika Kesi ya Rufaa Na. 2/2020, iliyofunguliwa Mahakama Kuu kupinga uamuzi huo, Rugemeleza Nshala, mwanaharakati huyo amerudishiwa uwakili wake.
Dk. Nshala amesema kuwa, uamuzi uliotolewa na jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo, leo tarehe 21 Juni 2021, umeamuru sakata hilo lirudiwe kusikilizwa upya katika kamati hiyo, ili kumpa Fatma nafasi ya kujitetea.
Sakata hilo liliibuka baada ya Prof. Kilangi kupeleka malalamiko mbele ya Jaji Kiongozi wa Tanzania, Dk. Eliezer Feleshi, yaliyodai Fatma ametoa matamshi yaliyoishutumu Serikali, wakati akitetea katika kesi ya kupinga uteuzi wake, iliyofunguliwa na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu.
“Tunashukuru tumeweza kufanikiwa katika hatua ya kwanza, Fatma amerudishiwa uwakili wake, kwa maana hiyo sasa ana haki ya kwenda kujitetea mbele ya Kamati ya Mawakili, katika siku itakayopangwa,” amesema Dk. Nshala.
Dk. Nshala ameongeza “mahakama imeagiza msajili wa Mahakama Kuu apeleke mwenendo wa kesi na mlalamiko yaliyowasilishwa na AG mbele ya Jaji Kiongozi, apeleke yale yale mbele ya kamati ya mawakili.”
Hata hivyo, Dk. Nshala amesema Fatma hataweza kuendelea na kazi ya uwakili, kwa kuwa uamuzi wa kusimamishwa uwakili wake, utaendelea kuwepo, hadi maamuzi ya kamati hiyo dhidi ya malalamiko hayo yatakapotolewa.
“Hawezi kuendelea na majukumu yake ya uwakili, sababu ile amri ya kumsimamisha bado ipo, iliyoondolewa ni ile ya kufuta uwakili,” amesema Dk. Nshala.
Jaji Feleshi alitoa uamuzi wa kumvua uwakili Fatma, pamoja na kuiondoa kesi hiyo iliyokuwa inapinga uteuzi wa Prof. Kilangi, Oktoba 2020.
Baada ya kumvua uwakili, Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), kilikata rufaa Mahakama Kuu kupinga uamuzi huo.
Leave a comment