KLABU ya Yanga imewatoa wachezaji wake Juma Mahadhi na Abdulaziz Makame kwa mkopo ufuatia kutopata nafasi kwenye kikosi hicho kwa sasa, sambamba na wachezaji wa timu ya vijana Adam Kiondo na Fahad Fuad ambao wanahitaji kupata uzoefu na muda mwingi wa kucheza. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea)
Kutolewa kwa mkopo wachezaji hao kunakuja kufuatia kufunguli kwa dirisha dogo la usajili hii leo tarehe 15 Desemba, 2020 kwa klabu za Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi daraja la kwanza.
Taarifa hiyo inakuja siku chache mara baada ya kocha wa kikosi hiko, Cedric Kaze kunukuliwa akisema kuwa timu yake inawachezaji wazuri ila kwa kuwa hawapati nafasi basi watalazimika kuwatoa kwa mkopo ili kutunza vipaji vyao.
“Kuna wachezaji wazuri lakini kwa kuwa hawapati nafasi katika kikosi cha kwanza tutawatoa kwa mkopo ili wakaendeleze vipaji vyao kwa kuwa ni kipindi cha usajili tunaweza kusajili na wakaendelea kukosa nafasi,” alisema Kaze.
Tayari Kaze ameshafanya ingizo jipya kwenye kikosi cha Yanga kwenye dirisha dogo la usajili toka alipokabidhiwa mikoba ya kuinoa timu hiyo kwa kumsajili Saidi Ntibazonkiza ambaye ataanza kuitumikia timu hiyo kwenye mchezo ujao wa Ligi Kuu utakaochezwa tarehe 19 Desemba, 2020 kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abed, jijini Arusha dhidi ya Dodoma Jiji.
Imeripotiwa kuwa Juma Mahadhi atajiunga na timu ya Ihefu FC yenye makao yake jijini Mbeya, ambayo imepanda Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu kwa mkopo wa miezi sita.
Yanga hii leo inatashuka dimbani kwenye mchezo wa kujipima nguvu dhidi ya Singida United inayoshiriki Ligi daraja la kwanza, mchezo huo utachezwa kwenye Uwanja wa Malkia Liti zamani ukifahamika kwa jina la Namfua.
Leave a comment