RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli, amesema atafanya uteuzi mpya wa Naibu Waziri wa Madini baada ya aliyemteua, Francis Ndulane kushindwa kuapa. Anaripoti Brightnes Boaz, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema hayo leo Jumatano tarehe 9 Desemba 2020, muda mchache baada ya kumaliza kuwaapisha mawaziri na naibu mawaziri, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
Rais Magufuli amesema hayo, wakati akichambua wizara moja baada ya nyingine pamoja na mawaziri na naibu wao.
“Ninawafahamu wote niliowateua, mpaka wewe uliyeshindwa kuapa. Nafikiri nitamtafuta mwingine anayejua kuapa vizuri. Tunakupongeza utaendelea kuwa mbunge na tutacheki vizuri shahada yako,” amesema Rais Magufuli.
Amesema, lazima kuwe na naibu waziri anayeweza kusoma vizuri nyaraka mbalimbali ili asije kusaini nyaraka za muhimu bila kusoma kwa umakini.
Wakati wa kiapo, Kumba alikuwa akikosea kusoma kiapo kwa kurudia rudia hali iliyomfanya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi kumpa maelekezo.
Hata hivyo, Ndulane ambaye ni Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM) hakumaliza kiapo chake kwa Balozi Kijazi kumwomba aende akampumzike kwanza ili kupisha wengine kuendelea kuapishwa.
Kwa mujibu wa wasifu wa Ndulane uliowekwa katika tovuti ya Bunge la Tanzania, inamwonyesha ana shahada ya uzamili ya uhasibu na fedha aliyoipata Chuo Kikuu cha Mzumbe kati ya mwaka 2013 hadi 2015.
Leave a comment