RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam, kuhakikisha inamaliza tatizo la wanafunzi wa Shule ya Msingi, Barango, Halmashauri ya Ubungo kukaa chini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Bukoba…(endelea).
Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo Jumatatu tarehe 18 Januari 202, wakati akizindua majengo ya Shule ya Wavulana Ihungo iliyoko Bukoba Mkoa wa Kagera.
Uzinduzi huo, umefanyika baada ya kufanyiwa ukarabati uliogharimu Sh.10.9 bilioni kutokana na kuharibika kufuatia tetemeko la ardhi lililotokea tarehe 10 Septemba 2016.
Katika uzinduzi huo, Rais Magufuli amewaomba viongozi wenzake ndani ya Serikali “mahali ambapo kuna mapungufu mbalimbali tuyashughulikie. Nimefurahi kuambiwa hapa makupungu mengi tumeyamaliza.”
“Lakini kuna maeneo hata Dar es Salaam, kuna mapungufu, kuna shule moja ya msingi Ubungo Dar es Salaam inaitwa Barango, ina wanafunzi wengi tu, shule hiyo iko Dar es Salaam, Ubungo bado wanakaa chini,” amesema Rais Magufuli.

“Madarasa mengine yamebomoka, madawati yamevunjika na yamechwa, mkuu wa wilaya yupo, mkuu wa mkoa yupo, mkurugenzi yupo bado anakusanya kodi na mbunge wa Ubungo yupo tena yupo hapa ni profesa (Kitila Mkumbo) ni wa elimu, ” amesema Rais Magufuli huku akimwita mbele Profesa Kitila ambaye ni Waziri wa Uwekezaji ili wananchi wamwone
“Simama hapa Profesa wananchi wako wa Ubungo wakuone.”

Akiendelea kuzungumza amesema, “lakini hiyo shule ya Ubungo Barango wanakaa chini, namshukuru huyo mwandishi kaitoa mitandaoni, viongozi wa huko wakasema ni masuala ya kisiasa, siyo kisiasa mimi ndiyo napenda kuyajua.”
“Nazungumza nikiwa Kagera, nikienda Dar es Salaam, niyakute hayo madarasa yamekamilika na hawakai chini, nitakwenda kuitembelea mimi hiyo shule na kama wananisikiliza ‘message sent and deleted” amesema
Katika kusisitiza hilo, Rais Magufuli amesema “haiwezekani uwe umechaguliwa na wananchi unaitwa Rais na wewe ukawapa watu madaraka, ukawapa uwaziri, ukuu wa mkoa, ukurugenzi na wanakusanya kodi na bajeti zipo na wanazunguka kwenye maeneo hayo, unakuta wanafunzi wanakaa chini, wao wanazunguka, hii ni dhambi kwangu kwamba nilikosea kuwachagua baadhi ya viongozi.”
Rais Magufuli amesema, kuna baadhi ya maeneo hawafanya kazi vizuri hasa kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
Leave a comment