MGOMBEA urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), RAIS John Pombe Magufuli amewashangaa watu wanaompinga Dk. Phillip Mpango katika Jimbo la Buhigwe mkoani Kigoma katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Dk. Mpango ambaye kwa sasa ni Waziri wa Fedha na Mipango anagombea Ubunge BUhigwe kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Jimbo hilo lilikuwa likiongozwa na Albert Obama wa CCM ambaye alishindwa kutetea nafasi hiyo kwenye kura za maoni na Dk. Mpango akaongoza na vikao vya juu ya chama hicho vikamteua kugombea ubunge.
Dk. Mpango alipata fursa ya kuwa waziri baada ya kuteuliwa na Rais Magufuli kuwa mbunge wa kuteuliwa mwaka 2015 kisha kumteua tena kuwa waziri.

Soma zaidi: Magufuli avunja ukimya fedha tetemeko Kagera
Akizungumza katika Mkutano wa kampeni za urais CCM zilizofanyika kwenye Uwanja vya Lake Tanganyika mkoani Kigoma leo Ijumaa tarehe 18 Septemba 2020, Rais
Magufuli amesema, kuna watu jimboni humo hawataki Dk. Mpango awe Mbunge licha ya kwamba amewaletea maendeleo.
“Dk. Mpango najua wanakusumbua huko jimboni kwako, lakini nasikia wameshaanza kumpinga tena kule wapinga maendeleo. Watu wa Buhigwe mnataka nini?” amehoji Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema, kama wananchi wa Buhigwe wanaijua thamani ya Dk, Mpango watamchagua au watampitisha bila kupingwa.
Amesema, baada ya kumteua kuwa mbunge na kufanya kazi nzuri, ulipowadia uchaguzi wa mwaka huu nilimwambia “Dk. Mpango nenda huko huko Kigoma ukaombe kura, ukaeleze yaliyofanyika wananchi wa Kigoma katika jimbo lako la Buhigwe.”
“Wanabuhigwe kama wanajua thamani yako watakupa kura na inawezekana wakakuopitisha bila hata kupingwa,” amesema Rais Magufuli.
Akielezea mambo ambayo Dk. Mpango ameyafanya akiwa Waziri wa Fedha, ikiwemo kusimamia ujenzi wa miradi ya barabara.
Leave a comment