RAIS John Magufuli ameonesha dhamira ya kutaka Job Ndugai, Mbunge wa Kongwa kuchaguliwa tena kwenye kiti hicho wakati wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Akizungumza kwenye ziara yake mbele ya wananchi katika Jimbo la Kongwa, jijini Dodoma Rais Magufuli amesema kuwa, Ndugai ambaye pia ni Spika wa Bunge anatosha.
Kwamba, amekuwa akiliongoza jimbo hilo vizuri huku akilisaidia taifa kutokana na nafasi yake aliyo nayo (Spika wa Bunge). Amewaeleza wanakongwa kwamba, atashangaa kama wale waliopambana na Ndugai mwaka 2015, watarejea kupambana naye mwaka 2020.
Rais Magufuli alitoa kauli hiyo tarehe 18 Julai 2019 jijini humo ikiwa ni baada ya Ndugai kumweleza (Rais Magufuli) kwamba, wananchi wa jimbo hilo wanasubiri 2020 wampe shukrani kwa kumpigia kura.
Akieleza zaidi Spika Ndugai alisema, wananchi hao watatumia sanduku la kura kutoa shukrani zao kwa Rais Magufuli. Mwaka 2020 kunatarajiwa kufanyika uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani.
Akionesha dhamira ya kutaka kufanya kazi na Ndugai 2020 endapo atakuwa rais kwa awamu ya pili, Rais Magufuli alishauri wale walioingia kwenye kura za maoni na mbunge huyo (Ndugai) 2015, waachane na fikra hizo.
“… lakini ninawambia kuwa, mmechagua mtu ambaye anasaidia nchi nzima kwa nafasi yake na msingemchagua kuwa mbunge kwa vyovyote asingekuwa spika. Ninafahamu wakati wa kampeni kulikuwa na wengine waliohitaji ubunge.
“…, na nilipofika hapa niliwaambia kazi si ubunge na ukweli ni kwamba, wale wote waliogombea niliwateua nafasi mbalimbali wengine wakawa wakurugenzi na wengine wakuu wa mikoa hivyo, nitashangaa sana kama 2020 watakuja tena kugombea hapa,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment