RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli, amewapunguzia adhabu wafungwa 256 waliohukumiwa kunyongwa na kuagiza wapewe kifungo cha maisha gerezani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wafungwa hao ni wale waliohukumiwa kunyongwa katika uongozi wa muhula wa kwanza wa Rais Magufuli.
Rais Magufuli ametangaza uamuzi huo leo Jumatano tarehe 9 Desemba 2020, katika hafla ya uapisho wa mawaziri 21 na manaibu waziri 23, iliyofanyika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
“Leo ni siku ya Uhuru, najua katika kipindi cha miaka mitano mpaka leo natakiwa niwe nimenyonga watu 256 waliohukumiwa kunyongwa, sijanyonga hata mmoja, na wale 256 kwa mamlaka niliyopewa, nawapunguzia kifungo cha kunyongwa, sasa wafungwe maisha,” ameagiza Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema “watanyongwa na wengine, sijui Jaji Mkuu (Prof. Ibrahim Juma), inawezekana huyo atakayekuja atawanyonga.”
Rais Magufuli amesema ameshindwa kuchukua hatua hiyo kwa kuwa hataki kuwa muuaji.
“Sababu hao waliohukumiwa kunyongwa waliua, mimi sheria iliniambia niue 256, nani mwenye dhambi zaidi huyo alioua mmoja au mimi nitakaoua 256?” amehoji Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema “Nimeshindwa ninaomba mnisamehe kwenye hilo, kwamba mimi nitakuwa muuaji, sababu wenzangu waliua wawili, mmoja au watatu walihukumiwa kunyongwa.”
Wakati huo huo, Rais Magufuli, amewapunguzia adhabu na kuwaacha huru baadhi ya wafungwa kati ya wafungwa 3,316, waliopendekezwa kwake na Kamishna Jenerali wa Magereza.
“Wako wengine 3,316 wana makosa madogo ya wizi wa kuku, wengine walitumikia kifungo chao kwa muda mrefu. Kwa mujibu wa mapendeko yaliyoletwa na Kamishna Jenerali wa Magereza, nimekubali kuwapunguzia adhabu zao na wengine kuachiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Rais Magufuli.
Kiongozi huyo wa Tanzania ameagiza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kushughulikia suala hilo.
“Wizara ya Mambo ya Ndani kasimamieni hili kwa mujibu wa sheria, hao wakafungwe maisha wakashiriki katika kufanya kazi,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment