JOHN Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amefuta mawazo kwamba, nchi hii haiwezi kuongozwa na chama kingine isipokuwa Chama Cha Mpinduzi (CCM) pekee. Anaandika Regina Mkonde.
Kauli hiyo inanonesha kwamba, si yeye wala CCM iliyo tayari kuachia madaraka hata kama watashindwa na chama cha upinzani kwa njia ya kidemokrasia.
Rais Magufuli ametamka kauli hiyo huku kukiwa na mgogoro wa kisiasa visiwani Zanzibar uliotokana na CCM kushindwa na Chama cha Wananchi (CUF) kwenye uchaguzi uliofanyika tarehe 25 Oktoba mwaka jana na baadaye matokeo hayo kufutwa.
Rais Magufuli amesema hayo leo kwenye maadhimisho ya miaka 39 ya CCM katika viwanja vya Namfua mkoani Singida.
“Wapinzani wasitegemee siku moja watakuja kuiongoza nchi, marufuku! Na wananchi waache kuwaza vyama vingine vya ovyo ovyo na ajabu bali watuamini kwa kuwa tumejipanga,” amesema.
Rais amesema kuwa, vyama vya upinzani visiweke matumaini ya kuishika nchi na kuwa, CCM iko imara, jeuri na hakuna wa kuikwamisha.
Pia kwenye mkutano huo, Rais Magufuli amesema kwamba, watendaji wa serikali kuanzia ngazi ya chini hadi juu wasioweza kutekeleza Ilani ya CCM, waachie ngazi.
Amesema “uongozi wa serikali yangu tumeamua kuitekeleza Ilani ya CCM kikamilifu ili kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi. Watendaji wa serikali kuanzia ngazi ya chini hadi juu wasioweza kutekeleza Ilani wakae pembeni.”
Pia ameonya wakuu wa wilaya, mikoa, mawaziri, watumishi na watendaji wa serikali kuwa watawajibishwa endapo watashindwa kutatua kero za wananchi ipasavyo hasa zilizoandikwa kwenye Ilani ya CCM.
“Uongozi wa serikali yangu unawathibitishia Watanzania kuondoa kero zao, tumedhamiria kufanya kazi na tutaifanya kazi,” amesema.
Amesema serikali yake itaendelea kutoa ushirikiano kwa CCM sababu hakuna serikali yenye maendeleo bila ya uwepo wa CCM.
“Serikali ninayoongoza itaendelea kuonesha ushirikiano na CCM kwasababu hakuna serikali bila ya CCM. Nasisitiza tena, watakaoshindwa kuitekeleza Ilani ya CCM watatupisha kwa nguvu ili waingie watakaoweza,” amesema.
Ameipongeza CCM kwa kutoa msaada wa madawati 1,000 ambayo yatasambazwa kwenye Halmshauri za Mkoa wa Singida na kwamba, itaondoa changamoto ya wanafunzi kukaa chini.
Amesema serikali imejipanga kuondoa changamoto zinazojitokeza sasa, hasa ya ongezeko la idadi ya wanafunzi walioandikishwa ambayo haiendi na idadi ya madarasa.
“Kila jambo zuri lina changamoto zake, wananchi wameitikia wito wa serikali wa kupeleka watoto shule, kitendo kilichopelekea idadi ya wanafunzi kuongeza ukilinganisha na madarasa yaliyopo,” amesema na kuongeza;
“Serikali iko mbioni kuondoa changamoto hiyo na nyingine zitakazojitokeza ili kufanikisha adhma yetu ya kutoa elimu bure kwa wanafunzi kuanzia Darasa la 1 hadi Kidato cha Nne.”
Kwenye mkutano huo, Jakaya Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa CCM amesema Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kuwa ana uwezo wa kutekeleza majukumu ya rais inavyostahili.
Dk. Kikwete ambaye ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne amesema,“CCM haikufanya makosa kumchagua Samia Suluhu kuwa makamu wa kwanza wa rais mwanamke kwasababu ana uwezo wa kutekeleza majukumu ya rais pale anapokuwa na udhuru.” amesema Dk. Kikwete na kuongeza;
“Kama una uwezo wa kutekeleza majukumu ya rais vilivyo anapopata udhuru, utashindwaje kuyatekeleza utakapo kuwa Rais?,” amesema.
Amesema kuwa CCM imefuata misingi ya usawa wa kijinsia kwa kumchagua mwanamke kuwa makamu wa rais na kuvunja rekodi ya kuwa chama kinachothamini mchango wa wanawake kwenye maendeleo ya Taifa.
Hata hivyo amesema, amefurahishwa na utendaji kazi wa Serikali ya Rais Magufuli na kuwa, awali chama kilikuwa kwenye wakati mgumu hivyo atakiimarisha na kuwarudishia matumaini wananchi.
“Mimi naamini viongozi wazuri wapo kwenye chama chetu, tuwashauri wagombee, waliochokaa wakae pembeni ili wanaoweza wafanye kazi ya kuimarisha chama,” amesema.
Kichekesho! Hivi elimu bure inatokana na walimu kuzuiwa kupokea michango moja kwa moja kutoka kwa wazazi, au inatokana na serikali kubeba mzigo wa michango ya wazazi? Hivi kuhamishia udhibiti wa michango ya wazazi kwa kamati ya chakula ya wazazi wenyewe badala ya uongozi wa shule kunaifanya michango hii kutokuwa na thamani kiasi cha kuilinganisha na bure? Yaani mzazi akitoa mchango wa chakula cha mtoto wake shuleni, anakuwa amechangia; Lakini akitoa mchango huo huo kwa kamati ya chakula inayosimamiwa na wazazi wenyewe, anakuwa hajachangia chochote na mtoto wake anakuwa anapata elimu bure! Kichekesho! Sidhani kama jambo hili limeamuliwa na watu wazima waliokwenda shule, sidahani.