RAIS John Magufuli amechukua fomu ya kuomba kuteuliwa na Chama cha Mapinduzi (CCM), kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Rais Magufuli ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM, amekabidhiwa fomu hiyo leo Jumatano tarehe 17 Juni 2020 jijini Dodoma na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa chama hicho.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa fomu hiyo, Rais Magufuli amesema anaanza mapema mchakato wa kutafuta wadhamini 250, ili awahi kurejesha fomu hiyo mapema.
Mwenyekiti huyo wa CCM amesema amekuwa akipigiwa simu na makada wa chama hicho, ambao wamemuahidi kumdhamini.
“Naomba nianze zoezi hili la kutafuta wadhamini, nitaenda mikoa yote kwa sababu nimekuwa nikipigiwa simu wakisema wanataka kunidhamini hivyo nitarejesha fomu yangu kwa wakati,” amesema Rais Magufuli.
Kama atapitishwa na CCM kugombea kwenye uchaguzi huo, Rais Magufuli atachuana na wagombea wa vyama vya siasa vya upinzani, kwa ajili ya kutetea kiti chake cha urais, alichoketi kuanzia mwezi tarehe 5 Novemba 2015.
Leave a comment