WATU watano wamefariki dunia, katika ajali iliyohusisha magari matatu ikiwemo basi dogo la abiria ‘Costa’ iliyotokea eneo la Nanenane mkoani Morogoro jana Jumatatu usiku, tarehe 22 Juni 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Fortunatus Musimu amesema, ajali hiyo imehusisha magari matatu moja likiwa gari la abiria aina ya Toyota Costa lenye namba za usajili T689 DUK liliyokuwa linatokea jijini Dar Es Salaam kuelekea Morogoro.
Amesema, gari hilo liligonga gari dogo aina ya Toyota Cresta T563 ASA na baadaye Costa hilo kugongana uso kwa uso na lori la kampuni ya Dangote yenye namba za usajili T658 DJZ.
Kamanda Musilim amesema, chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa gari la abiria aina ya Toyota Costa kutaka kulipita gari dogo aina ya Toyota Cresta ambapo gari hilo lilipoteza uelekeo na kwenda kugongana ana kwa ana na lori la kampuni ya Dangote na kusababisha vifo vya watu watano huku majeruhi wakikimbizwa hospitali kwa matibabu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Albert Msando ametoa rai kwa madereva kufuata kanuni na sheria za barabarani.
Pia, amewaasa abiria kuchukua tahadhari hasa wanapoona mwenendo wa dereva hauridhishi ili kuepuka ajali kama hizo ambazo zinapotea nguvu kazi ya taifa.
Leave a comment