MAELFU ya waombolezaji wamefurika katika viunga vya barabara ya Ali Hassani Mwinyi na Kawawa mkoani Dar es Salaam, kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli (61). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tukio hilo la kuhuzunisha limetokea leo Jumamosi asubuhi tarehe 20 Machi 2021, baada ya mwili wa Hayati Magufuli kutoka Kanisa Katoliki la St. Peter’s kulikofanyika Ibada fupi.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa ibada hiyo, Msemaji wa Familia, Ngusa Samike amesema, Dk. Magufuli alipata fursa za kupata ukapo wa wagonjwa uliyoongozwa na Kardinali Polycarp Pengo pamoja na Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zuberi.
Samike amesema, Dk. Magufuli ‘’aliwaongoza manesi na madaktari kwa sala na kwa nyimbo na tunashukuru kwa sala za mwisho wa mpako wa wagonjwa. Tunamshukuru Kardinali Pengo na Mufti kwa sala.’’
Mara baada ya kumalizika kwa Ibada hiyo, mwili huo ulipelekwa Uwanja wa Uhuru mkoani Dar es Salaam, kunakiofanyika shughuli ya kuuaga leo na kesho Jumapili.
Waombolezaji hao walijazana maeneo ya barabara ulipoputa msafara wenye mwili wa Dk. Magufuli huku baadhi yao wakiumwagia mauua na wengine wakitandika khanga barabarani na wengine wakiwa na matawi ya miti.
Vilio na majonzi, vilishamili pindi gari lenye mwili wa Dk. Magufuli ukipita mbele yao na wengine wakibubujikwa machozi.
Hayati Rais Magufuli alifariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu ya matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo.
Mwili wa Hayati Magufuli unatarajiwa kuagwa Dar es Salaam kwa siku mbili (Jumamosi na Jumapili), kisha tarehe 22 Machi 2021, mwili huo utaagwa katika Makao Makuu ya nchi Dodoma.
Tarehe 23 Machi 2021, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa visiwani Zanzibar, kisha utasafirishwa Mwanza kwa ajili ya shughuli ya kuuaga tarehe 24 Machi 2021.
Baada ya kuagwa Mwanza, mwili wa Hayati Rais Magufuli utaagwa na wananchi wa Chato mkoani Geita, tarehe 25 Machi mwaka huu.
Baada ya mwili huo kuagwa Chato, shughuli za mazishi zitafanyika tarehe 26 Machi 2021, kijijini kwao Chato mkoa Geita
Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV na MwanaHALISI Online kwa habari zaidi
Leave a comment