BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro limeunda Kamati maalum ya kuchunguza upotevu wa kiasi cha Sh. 353 milioni ambazo hazikuingizwa kwenye akaunti maalum ya Halmashauri. Anaripoti Christina Haule … (endelea).
Mwenyeiti wa Baraza hilo Kibena Kingo amesema hayo wakati akitoa maazimio ya kikao hicho kwenye kikao maalum cha baraza la Madiwani kilichofanyika katika ukumbi uliopo wilayani humo.
Kingo amesema kuwa kamati hiyo maalum itafanya kazi ndani ya wiki moja kuanzia Juni 17 hadi 23 ili kuchunguza fedha hizo zimepotelea wapi na kuondoa mashaka yaliyopo ndani ya wajumbe wa baraza hilo.
Awali wajumbe wa Baraza hilo akiwemo Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, Omari Mgumba walihoji kuhusiana na taarifa ya mapato na matumizi ya Halmashauri hiyo iliyohakikikiwa na mkaguzi wa ndani kuonesha upotevu wa fedha hizo huku ikimaanisha kuwa fedha hizo hazijaingizwa kwenye akaunti kwa muda wa mwaka mzima bila wahusika kuchukuliwa hatua yoyote mapema.
Mgumba amesema kuwa fedha hizo pia zimeshindwa kuingizwa kwenye akaunti yake licha ya kikao cha ndani cha baraza hilo kuagiza kwa kutoa masaa 72 tangu Juni 5 mwaka huu kuwa fedha hizo ziwe zimeingizwa na kuondoa utata huo jambo linaloonesha kuwa kuna ujanja wa watu wachache.
Hivyo Mbunge huyo amesema kuwa akishirikiana na kamati hiyo atahakikisha kuwa wanabaini upotevu huo umetokea wapi na kuwabaini wahusika na kisha kuwafikisha kwenye baraza lijalo kwa ajili ya kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria zilizopo.
Kikao hicho kilichohudhuriwa na madiwani wa kata zote na wabunge wake kilifikia tamati pia ya Kuiomba Serikali kupitia Wizara ya miundombinu kuhakikisha inawabadilishia Meneja wa wakala wa barabara vijijini (TARURA) kufuatia aliyekuwepo kushindwa kutoa ushirikiano kwa wajumbe wa barabara hilo na viongozi wa wilaya licha ya kuharibu kazi katika wilaya hiyo.
Leave a comment