MADIWANI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Makurumla Manispaa ya Ubungo, Bakari Kimwanga na mwenzake wa Mzimuni Manispaa ya Kinondoni, Manfred Lyoto jijini Dar es Salaam, wamebaini uchafuzi wa mazingira mfereji wa mpaka unaotenganisha kata zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika ziara yao walioifanya jana Alhamisi tarehe 28 Januari 2021, madiwani hao wakiwa wameambatana na wenyeviti wa mitaa ya Mtambani, Abdullah Kitumbi na Ibrahim Mselemu wa Kimamba, walikagua mfereji huo ambao walibaini nyumba nyingi zilizopo kando ya mfereji huo, zimeunganisha mabomba ya maji machafu ikiwamo kutiririsha maji taka.
Akizungumzia hali hiyo, Kimwanga alisema, katika kipindi hiki ambacho mvua zipo karibuni kuanza ni lazima mrefeji huo usafishwe kwa kuwashirikisha wananchi.
“Ni aibu, kwani yapo mambo ambayo wenyeviti wa mitaa mnatakiwa kuuangalia badala ya kukaa ofisini. Hivyo, tumeona namna baadhi ya wananchi wameunganisha mabomba ya maji taka jambo ambalo ni hatari kwa afya zao,” alisema Kimwanga.
“Tunachoomba wenyeviti, kutaneni haraka mpange kikao cha pamoja ambacho kitashirikisha wananchi wa pande mbili na hiki kikao mtuarifu mapema mimi na mwenzangu (Lyoto) tutahudhuria,” alisema Kimwanga.
Kwa upande wake, Lyoto, alisema ipo haja kusafishwa kwa mfereji huo ikiwamo kuomba nguvu ya pamoja kwa Manispaa ya Ubungo na Kinondoni.
“Yapo maeneo yanahitaji nguvu kazi ya wananchi na mengine ni lazima tusafishe mfereji kwa kutumia burudoza,” alisema Lyoto.
Leave a comment