NAIBU Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi nchini Tanzania, Angeline Mabula ameagiza watu wote wanaoishi nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakiwa sio wapangaji kwa mkataba, wajitokeze ili kupangishwa rasmi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro…(endelea).
Amesema, Serikali inakusudia kuchukua hatua kali dhidi ya wapangaji waliosaini mikataba lakini wakapangisha watu wengine hatua inayolinyima shirika mapato.
Naibu waziri huyo amesema, wapangaji waliofanya hivyo ni wahujumu uchumi wa shirika na hawatovumiliwa.
Amesema hayo leo Jumatatu, tarehe 29 Novemba 2021, wakati akifungua mkutano wa ushirikiano wa kikazi na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) unaofanyika Hoteli ya Nashera, mjini Morogoro.
Shirika la Nyumba la Taifa linadai wapangaji wake Sh.26 Bilioni nchi nzima na hivyo kuchangia kupunguza kasi ya ukuaji wake kiuchumi.
Katika mipango yake, shirika limepata miradi minane ya kujenga majengo ya kisasa ya wizara mbalimbali huku likiendelea na mradi wa kujenga nyumba 1,000 za makazi jijini Dodoma, ikianzia na nyumba 400.
Kwa jumla Tanzania inakabiliwa na upungufu wa nyumba milioni tatu za makazi.
Shirika lilianzishwa mwaka 1962 kwa lengo la kujenga nyumba bora na mwaka mmoja baadaye lilifanikiwa kujenga nyumba 14,845 chini ya operesheni maalum ya “Ondoa Makuti.”
Leave a comment