WAKATI maandamano yaliyoitishwa na Chama cha upinzani Afrika Kusini, Economic Freedom Fighters, yakiendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali , Ubalozi wa Tanzania nchini humo, umewataka Watanzania kutojihusisha nayo pamoja na kuchukua tahadhari. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Tahadhari hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 20 Machi 2023 na Ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, kwa watanzania waishio nchini humo.
“Kama mlivyosikia na kuona kwenye vyombo vya habari vilivyopo nchini Afrika Kusini, leo siku ya Jumatatu ilipangwa kuwa siku ya maandamano na mgomo wa kitaifa nchi nzima na kulingana na taarifa zilizopo maandamano hayo yanaendelea sehemu mbalimbali,” imesema taarifa hiyo na kuongeza:
“Kwa muktadha huo Ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini unawasihi watanzania waishio nchini hapa kuchukua tahadhari, kuwa watulivu na kujiepusha na kujihusisha kwa namna moja au nyingine katika matukio haya. Aidha, tunasisitiza mawasiliano na kutoa taarifa ubalozini kupitia viongozi wa jumuiya, tukio lolote litakalowahusisha watanzania wenzetu.”
Maandamano hayo yaliitishwa na chama hicho cha pinzani kikimtaka Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, ajiuzulu kwa madai kwamba ameshindwa kuimarisha uchumi wa taifa hilo.
Hatua hiyo imejiri baada ya Afrika Kusini kukabiliwa na changamoto ya hali ya uchumi, ukosefu wa ajira na madai ya uwepo wa ufisadi na kukatika umeme mara kwa mara.
Leave a comment