MKUTANO Mkuu wa chama cha siasa cha upinzani nchini Tanzania cha ACT-Wazalendo, kimewateua Bernard Membe na Maalim Seif Sharif Hamad kuwa wagombea urais wa Tanzania na Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Membe na Maalim Seif wameteuliwa leo Jumatano tarehe 5 Agosti 2020 katika mkutano mkuu huo uliofanyikia ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam.
Akitangaza matokeo hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Joran Bashange amesema, wajumbe walikuwa 428 ambapo waliopoga kura kumteua mgombea urais wa Tanzania walikuwa 420.
Bashange amesema, Membe aliyewahi kuwa waziri wa mambo ya nje wa Tanzania amepata kura 410 sawa na asilimia 97 huku kura kumi zikimkataa.
Nafasi ya mgombea urais wa Zanzibar, Bashange amesema, waliopiga kura walikuwa 420 ambapo kura 419 ni za ndio sawa na asilimia 99.6 na kura moja imemkataa.
Hii ina maana kwamba, Maalim Seif Sharif Hamad atakwenda kuchuana na wagombea wa vyama vingine akiwemo Dk. Hussein Ali Mwinyi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Pia, Membe atakwenda kuchuana na wagombea wengine wakiwemo Rais John Pombe Magufuli wa CCM na Tundu Lissu wa Chadema.
Hata hivyo, kuna uwezekano Membe na Lissu mmoja akamwachia mwenzake asimame kugombea urais ili mmoja amuunge mkono mwenzake.
Tayari, viongozi wa ACT-Wazalendo na Chadema wamekwisha weka wazi kwamba wako kwenye majadiliano ya jinsi ya kushirikiana.
Leave a comment