SIASA za kukomoana zimetamalaki Zanzibar na hiki ndicho kilichosababisha viongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar kusota rumande bila sababu za kueleweka. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Zanzibar … (endelea).
Kauli hiyo ilitolewa na Maalim Seif Shariff Hamad, mshauri mkuu wa Chama ACT Wazalendo katika kongamano la kuadhimisha miaka tisa ya kuasisiwa kwa mfumo wa serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK) lililofanyika tarehe 31 Julai 2019.
“Kitendo cha Masheikh wa Uamsho kuendelea kusota rumande jijini Dar es salaam kwa miaka sita bila sababu ya msingi, ni matokeo ya siasa za kukomoana zilizotamalaki Zanzibar baada ya kuhujumiwa kwa maridhiano ya Wazanzibari,” amesema Maalim Seif.
Viongozi wa Uamsho walikamatwa mwaka 2012 visiwani Zanzibar kwa madai ya kusababisha vurugu na kuhifadhi magaidi.
Akifafanua zaidi athari zinazotokana na kuvunjwa kwa maridhiano hayo, Maalim Seif alisema, baadhi ya jamaa, ndugu na hata marafiki wa viongozi hoa wamekuwa wakitishwa.
Ni wale ambao wamekuwa wakifuatilia taarifa na mwenendo wa suala la viongozi hao wa dini na maarufu visiwani humo.
Tarehe 31 Julai 2010, Wazanzibari kupitia kura ya maoni, zaidi ya asilimia 60 ya Wazanzibari walichagua kuongozwa kwa mfumo wa serikali ya umoja wa kitaifa.
Kwa mara ya kwanza iliundwa baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 2010 na kuongozwa na Dk. Ali Mohammed Shein ambapo Maalim Seif akiwa Makamu wa Kwanza wa Rais.
Hatua hiyo ilifikiwa baada ya Maalim Seif akiwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), kukutana kwa faragha na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume na kukubaliana kufuta siasa chafu za ubaguzi chuki na uhasama. Mkutano wao ulifikia kilele tarehe 5 Novemba 2009.
Leave a comment