MAALIM Seif Shariff Hamad, Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo, amewasihi Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Jabir Idrisa, Zanzibar … (endelea).
Maalim Seif ametoa wito huo leo tarehe 27 Machi 2020, wakati akihojiwa na Kituo cha Redio cha Bomba FM, Visiwani Zanzibar.
Maalim Seif amewaomba wananchi wote kufuata maelekezo yanayotolewa na watalaamu wa afya, kwa ajili ya kudhibiti ueneaji wa ugonjwa huo.
“Wananchi wote wa Tanzania tudumishe usafi, hakikisha kila mara tukoshe mikono yetu kwa kutumia maji tiririka na sabuni, tuepuka sana mikusanyiko, natoa Wito kwa Madereva wa dala dala kuhakikisha wanapinguza ujazaji wa abiria ili kutowa nafasi yakuepusha mbanano,” ameshauri Maalim Seif.
Wakati huo huo, Maalim Seif ameiomba Serikali ishirikiane na Vyama vya Siasa katika mapambano ya kudhibiti ugonjwa huo.
“Serikali ishirikishe vyama vya siasa katika vita hivi vya janga la Corona umoja wa kitaifa ni muhimu sana, tuache kuingiza tofauti za kisiasa, wito wangu tuwe wamoja. Tuko tayari kushirikiana na serikali zote mbili kupambana na janga hili la Corona,” amesema Maalim Seif.
Hadi sasa serikali imetangaza kwamba, kuna wagonjwa 13 wa COVID-19, ambao wanaendelea vizuri.
Leave a comment