MAALIM Seif Shariff Hamad, Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, hana kinyongo na Prof. Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Amesema, kuthibitisha hilo, tayari alikutana na Prof. Lipumba na kufanya naye mazungumzo pasi na tatizo lolote. Maalim Seif ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa chama hicho (CUF), aliondoka kutokana na mgogoro wa kiuongozi uliodumu kwa muda mrefu.
Mkongwe huyo wa siasa za upinzani Zanzibar na Makamu wa Pili wa Rais visiwani humo, ametoa kauli hiyo leo tarehe 15 Novemba 2019, wakati akifanya mahojiano katika kipindi cha Konani, kinachorushwa na Televisheni ya Mtandaoni ya ITV.
“Tunakutana, tunaongea na hakuna uhasama, hata Lipumba tumekutana, tunazungumza hatuna uhasama,” amesema Maalim Seif.
Maalim Seif ametoa kauli hiyo alipoulizwa kuhusu athari alizopata kufuatia hatua yake ya kuhama, alichohudumu kama Katibu Mkuu kwa muda mrefu.
Amesema, uamuzi huo ulimuathiri sana, kwa kuwa alikuwa anaipenda CUF, lakini kutokana na changamoto zilizojitokeza, amekubali matokeo.
“Bila shaka niliathirika, lakini nilisema mtu alikuwa na mtu wake amempenda lakini Mwenyezi Mungu amemuhitaji – amemchukua – lazima avumilie, atasikitika lakini atavumilia ataendelea na maisha,” ameeleza Maalim Seif.
Hata hivyo, amesema yeye na wafuasi wake, hawakushtushwa sana na uamuzi wa mahakama wa kumpa ushindi Prof. Lipumba, wa kuwa Mwenyekiti halali wa CUF, licha ya kutoungwa mkono na viongozi pamoja na wanachama wengi.
Maalim Seif amesema, walifanya mazungumzo na ACT-Wazalendo kabla ya kuondoka CUF, baada ya kuona dalili za kushindwa kupata muafaka wa mgogoro, wa kiuongozi ulioibuka kwenye chama hicho.
“Mimi niko shwari kabisa, hakuna hata mmoja miongoni mwetu aliyeanguka kwa presha, tulijua kabisa. Kama mahakama ikiamua hivi, sisi tutajiunga na vyama vingine, mazungumzo yalifanyika mapema sana.
“Lazima ujitayarishe kabisa kabisa, hasa kuna hujuma, unaweza ukahisi una haki lakini mahakama ikaamua vingine, na sisi tulisema tunaheshimu mahakama,” amesema Maalim Seif.
Leave a comment