KUNDI la waasi la wanamgambo la M23, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), wameirudisha kambi ya kijeshi mashariki mwa nchi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Taarifa kutoka ndani ya serikali na M23 zinasema, hatua ya kukabidhi kambi hiyo mikononi mwa serikali, kuoitia vikosi vya kulinda amani vya Afrika Mashariki, ni kutimiza ahadi yake ya kuondoka kutoka kwenye maeneo waliyoyanyakua na kuyadhibiti kwa miezi kadhaa.
Wakazi wa eneo hilo la mashariki, siku ya Ijumaa walielezea furaha yao wakati waasi hao walipokabidhi vifaa na kambi ya kijeshi ya Rumangabo.
Kambi ya kijeshi ya Rumangabo, ni moja ya kambi kubwa zaidi katika eneo la mashariki mwa mkoa wa Kivu kaskazini.
Hata hivyo wakazi hao wamesema, bado wametawaliwa na wasiwasi kwa maelezo kuwa “hakuna uhakika wa usalama wa kudumu.”
Hafla ya kukabidhi kambi hiyo ya Rumangabo kwa vikosi vya kulinda amani vya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EACRF), inaashiria mwanzo wa kuondoka kwa wapiganaji wa kundi la M23 kutoka kwenye mji wa kimkakati wa kijeshi wa Rumangabo, ulio kilomita 40 kaskazini mwa mji mkuu wa mkoa Goma, ambao waasi waliuteka mwishoni mwa mwezi Oktoba.
Kwa mujibu wa waandishi wa habari wa shirika la AFP walioruhusiwa kuripoti juu ya makabidhiano hayo, shughuli hiyo ilisimamiwa na vikosi vya Kenya vya kulinda amani vilivyopelekwa DRC na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, shughuli hiyo ya jana inafuataia makabidhiano kama hayo ya mwezi uliopita ya kambi ya Kibumba, iliyo karibu kilomita 20 kusini mwa Kongo.
Jenerali Emmanuel Kaputa Kasenga, naibu kamanda wa kikosi cha Afrika Mashariki, amesema kuwa kudhibiti tena kambi ya Rumangabo kunaashiria hatua muhimu katika juhudi zinazoendelea za kuleta amani na utulivu katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo, iliyokumbwa na machafuko ya napigano ya wenyewe kwa wenyewe.
Naibu kamanda huyo amesema vikosi vya Jumuiya ya Afrika Mashariki vitaendelea kusimamia utaratibu wa kurudishwa maeneo yaliyotekwa na waasi wa M23 na ameyataka makundi mengine kufuata utaratibu huo na kusalimisha silaha zao.
Kiongozi wa M23, Kanali Imani Nzenze alisema katika hafla hiyo ya Ijumaa, kwamba wao wanataka amani na wataendelea kujumuika katika mchakato huo wa kutafuta amani na ndio sababu kundi lake la M23 limeamua kukabidhi rasmi kambi ya kijeshi ya Rumangabo.
Viongozi wa kikanda walifanikisha kufikiwa makubaliano kati ya pande hasimu Novemba mwaka jana, hatua inayolifanya kundi la M23 likiondoka na kukabidhi maeneo waliyoanyakua hatua itakayowawezesha watu waliogeuka wakimbizi wa ndani kurejea katika makazi yao waliyoyakimbia.
Leave a comment