WAMILIKI 207 wa ardhi wanaodaiwa zaidi ya Sh. 200 Bilioni, wamepewa siku tisa kuanzia leo ili kukamilisha malipo hayo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
William Lukuvi, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amesema, kama wamiliki hao hawatofanya hivyo ndani ya muda huo, mali zao zote zitataifishwa na hatua za kisheria zitachukuliwa.
Lukuvi ametangaza msimamo huo leo tarehe 11 Juni 2019, wakati wa kikao maalum kati yake na wamiliki wa ardhi ambao ni wadaiwa sugu wa kodi ya ardhi pamoja na malimbikizo. Kikao hicho kimefanyika jijini Dodoma.
Akizungumza na wamiliki wa ardhi Lukuvi amesema kuwa, imekuwa ni desturi ya wamiliki wa ardhi kutokuwa tayari kulipa kodi ya ardhi wakati bajeti ya kulipa bili ya umeme na maji wanaitenga.
“Nawataka wote kulipa kodi pamoja na malimbikizo kufikia tarehe 20 Juni 2019, nawataka wadaiwa wote mliopo hapa na nje ya ukumbi huu, yoyote anayemiliki ardhi wawe wameplipa kodi si zaidi ya terehe 20 mwezi huu ili kukwepa aibu na fedheha, wote mnajua msingi wa biashara zenu ni ardhi, mmejenga ofisi kwenye ardhi,” ameagiza Lukuvi.
Katika kikao hicho Lukuvi amesema kuwa, ifikapo Julai Mosi mwaka huu, wadaiwa ambao hawatakuwa wamelipa madeni yao pamoja na malimbikizo, hatua kali za kisheria zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kutaifisha mali zao bila kujali cheo cha mtu au nafasi yake.
“Watakao shindwa kutaifisha mali zao, tutanadi viwanda, hatua hizi zitachukuliwa ili kulipa malimbikizo ya kodi zinazodaiwa, fedha zote hizi zinaingia hazina.
“Hatua ya kwanza ni kubatilisha umiliki watu wasiolipa bila kujali taasisi gani, tunampelekea Rais John Magufuli abatilishe umiliki. Pili, kukamata na kuuza mali kupitia madalali ambao tumewateua. Hivyo mtambue ulipaji kodi wa ardhi si hiari, ni takwa la kisheria,” amesema.
Katika kikao hicho Lukuvi amesema kuwa, kitendo cha wamiliki kushindwa kulipa kodi kwa wakati na malimbikizo, kunasababisha kukosekana kwa huduma muhimu kwa Watanzania.
Amesema, kila Mtanzania ambaye anamiliki ardhi, ni lazima alipe kodi bila kujali kuwa ni masikini au tajiri.
Mbali na mambo mengine amesema kuwa, msamaha wa kulipa madeni utafanyika baada ya kumaliza kulipa madeni ya nyuma na watakaopewa kipaumbele cha msamaha ni taasisi ambazo hazifanyi biashara.
Leave a comment