Saturday , 20 April 2024
Home Habari Mchanganyiko LSF yazindua mfumo wa kidigitali kutoa msaada kisheria
Habari Mchanganyiko

LSF yazindua mfumo wa kidigitali kutoa msaada kisheria

Spread the love

SHIRIKA linalofanya kazi ya kukuza upatikanaji haki nchini Tanzania, kupitia uwezeshaji wa kisheria, Legal Services Facility (LSF), limezindua mfumo wa kidigitali wa kusaidia wananchi kupata msaada wa kisheria. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).

Mfumo huo wa kidigitali umezinduliwa leo Jumanne, tarehe 15 Juni 2021 na Waziri wa Katiba na Sheria, Prof. Palamagamba Kabudi, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Prof. Kabudi, amesema mfumo huo utasaidia kusogeza karibu huduma ya msaada wa kisheria kwa wananchi, hasa walioko maeneo ya vijijini.

“Leo nimefurahi kuona LSF wamekuja na mfumo ambao utasogeza huduma karibu zaidi kwa wananchi, wanaohitaji huduma ya msaada na wasaidizi wa kisheria,” amesema Prof. Kabudi.

Waziri huyo wa Katiba na Sheria, amesema mfumo huo utasaidia kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia, hasa kwa wanawake na watoto, kwani makundi hayo yatapa msaada wa kisheria kwa haraka, wanapokumbwa ukatili huo.

“Naamini kupitia mfumo huu wananchi wengi wakiwemo kina mama na watoto, wataweza kupata msaada wa haraka zaidi pale wanapokutana na changamoto mbalimbali, zinazohusiana na kuminywa ama kukandamizwa kwa haki zao, kutokana na jinsia au umri wao,” amesema Prof. Kabudi.

Prof. Kabudi amesema, Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, itaendelea kushirikiana na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), ikiwemo LSF, kuhakikisha wananchi wanapata msaada wa kisheria.
“Naipongeza sana LSF kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika suala hili la kutafsiri sheria kwa lugha ya Kiswahili na kwa kuendelea kutekeleza mradi wake mkubwa nchini Tanzania,” amesema Prof. Kabudi na kuongeza:

“Ambao kwa kiasi kikubwa umeweza kusaidia maelfu ya wananchi walio kwenye mazingira magumu, hususani wanawake na watoto kupata haki zao kutokana na kazi nzuri inayofanywa na wasaidizi wa kisheria nchi nzima.”

Akielezea utendaji wa mfumo huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa LSF, Lulu Ng’wanakilala, amesema utapatikana katika simu za mkononi kupitia program ya ‘HAKI YANGU App’.

Ng’wanakilala amesema, huduma hiyo itapatikana nchi nzima, ambapo wananchi wataunganishwa na wasaidizi wa kisheria takribani 4,000, walioko maeneo yote Tanzania.

“Mfumo huo ni wa kwanza kubuniwa na wa aina yake nchini Tanzania, ambao utamsaidia mwananchi kuwasiliana moja kwa moja na msaidizi wa kisheria, au mtoa huduma za msaada wa kisheria, kupitia simu ya mkononi kwa kutuma ujumbe mfupi wa maneno au kupiga simu,” amesema Ng’wanakilala.

Amesema mfumo huo utasaidia kuongeza uelewa wa masuala ya kisheria wananchi.

“Kwa uzoefu wa LSF katika kutekeleza mradi wa upatikanaji wa haki nchini, tumeona kuwa wananchi walio wengi bado wanakumbana na changamoto mbalimbali, ikiwemo vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto,” amesema Ng’wanakilala.

Mtendaji huyo wa LSF ameongeza “hivyo njia hii itachochea upatikanaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa urahisi zaidi mahali popote kupitia simu ya mkononi.”

Mbali na uzinduzi wa mfumo huo, Ng’wanakilala amesema LSF itaendelea kushirikiana na NGO’s zaidi ya 200, zinazotoa huduma ya msaada wa kisheria nchi nzima, ili kuwasaidia wananchi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari Mchanganyiko

Wauguzi, madaktari 1000 kugawiwa mitungi ya Oryx Gas

Spread the loveKAMPUNI ya Oryx Gas na Taasisi ya Doris Mollel Foundation...

Habari Mchanganyiko

Tanzania yachaguliwa Makamu wa Rais Tume ya Shirika la Hali ya Hewa Duniani

Spread the love  TANZANIA kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)...

Habari Mchanganyiko

NEMC yaonya wanaojenga bila tathmini ya mazingira

Spread the loveBARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC),...

BiasharaHabari Mchanganyiko

NMB Pesa Akaunti yawavutia wakaguzi wa ndani Afrika

Spread the loveUbunifu wa bidhaa bora wa Benki ya NMB pamoja na...

error: Content is protected !!