Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa LRHC chamvaa tena Rais Magufuli
Habari za Siasa

LRHC chamvaa tena Rais Magufuli

Rais John Magufuli
Spread the love

MATUKIO ya ukiukwaji na uvunjifu wa haki za binadamu nchini, yameanza kuongezeka katika kipindi cha utawala wa Rais John Pombe Magufuli. Anaripoti Kelvin Mwaipungu… (endelea).

Ripoti za kitafiti zinaonyesha kuwa katika mwaka 2017, matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu yameongezeka ukilinganisha na mwaka 2016.

Ripoti ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), iliyotolewa Aprili mwaka huu na kusambazwa kwa wabunge wa Bunge la Muungano, wakati wa mkutano wa Bajeti inasema, “haki za kiraia na kisiasa zilivunjwa zaidi mwaka 2017.”

LHRC inasema, “pia haki ya kuishi, haki dhidi ya ukatili, haki ya kuwa huru na usalama wa mtu, uhuru wa kujieleza, uhuru wa kukusanyika na uhuru wa kujumuika, nazo zilivunjwa kwa kiwango kikubwa mno.”

Kunyimwa kwa haki hizi pia kuliathiri haki ya kushiriki katika utawala/serikali, hususani haki ndogo ya kushiriki katika masuala ya siasa.

Kituo kimetaja haki tano (5) zilizovunjwa, kuwa ni pamoja na mauaji yanayotokana na imani za kishirikina, mauaji ya kibiti na mauji mengine yanayotokea maeneo ya Pwani.

Haki nyingine zilizotajwa, ni haki dhidi ya ukatili wa kingono na kimwili, hasa kwa watoto – ubakaji na ulawiti – haki ya kuwa huru na usalama wa mtu; uuaji, utekaji na uteswaji unaofanywa na watu wasiojulikana, ukamataji kinyume na sheria, kushambuliwa kwa watu, kupotea kwa Mwanahabari Azory Gwanda.

Kuhusu uhuru wa kujieleza, ripoti inasema, “kuminywa kwa uhuru wa kutoa maoni, vitisho na bugudha kwa wanahabari, matumizi ya sheria zenye vifungu tata au kandamizi, ni miongoni mwa mambo ambayo yamefanyika mwaka 2017.”

LHRC inataja ukiukwaji wa uhuru wa kukusanyika na kujumuika, kuzuiwa mikutano ya kisiasa, kuminywa uhuru wa kujieleza na kukusanyika na hata kuingilia uhuru wa asasi za kiraia.

Kwa mujibu wa kituo hicho, lengo ku la ripoti yake, ni kueleza hali ya haki za binadamu kwa mwaka 2017, ikionesha uvunjifu wa haki hizo na jitihada zilizofanyika katika kuzilinda.

Taarifa kwa ajili ya kuandaa ripoti hiyo, kituo kinasema, zilikusanywa kwa njia mbali mbali, ikiwamo taarifa kutoka taasisi za serikali, mahakama, bunge, halmashauri na jeshi la polisi.

Aidha, wengine waliosadia kupatikana kwa taarifa hizo, ni waangalizi wa haki za binadamu, mashirika yasiyokuwa ya kiserikali ya kimataifa, wateja wa msaada wa kisheria, wasaidizi wa kisheria, vyombo vya kitaifa na kimataifa vinavyosimamia haki za binadamu na vyombo vya habari.

Ripoti ya haki za binadamu ya mwaka 2017, ambayo MwanaHALISI Online imeona nakala imebeba kurasa 34 na imegawanyika katika sehemu kuu mbili:

Kwanza, imelenga kuonyesha hali ya haki za binadamu kwa upande wa Tanzania Bara; na pili imeonyesha hali hiyo upande wa Zanzibar.

Sura ya kwanza ya ripoti, inaelezea kuhusu Tanzania kama nchi, ikigusia kwa ufupi historia, jiografia, idadi ya watu na mihimili ya dola.

Sura ya pili hadi sita, zinaelezea ukiukwaji wa haki mbalimbali za binadamu, ambazo ni haki za kiraia na kisiasa; kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.

Sura ya saba, imejikita katika haki za makundi maalum – wanawake, watoto, watu wenye ulemavu, wazee na watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI.

Sura ya nane, inaelezea madhala ya rushwa kwenye haki za binadamu. Sura ya tisa inaelezea mifumo ya ulinzi wa haki za binadamu na sura ya kumi, inaelezea masuala mengine ambayo yanagusa au kuathiri haki hizo.

Hii ni ripoti ya pili kutolewa na kituo hicho ikituhumu walioko madarakani kukiuka haki za raia wengine.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

error: Content is protected !!