EDWARD Lowassa, Waziri Mkuu aliyejiuzulu katika serikali ya awamu ya nne, amenadi kazi zinazofanya na Dk. John Magufuli, Rais wa Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Amesema, kazi inayofanya na Rais Magufuli inapaswa kupongezwa hasa kutokana na kukabiliana na watumishi wazembe hivyo kuifanya nchi kuwaka moto.
Akizungumza leo tarehe 20 Septemba 2019, katika mahafali ya Shule ya Msingi Meyers, Arusha amesema, Rais Magufuli anastahili kupongezwa.
“Rais Magufuli anastahili pongezi, anafanya kazi nzuri. Tunaona mawaziri nao wanafanya kazi nzuri,” amesema Lowassa huku akimtaja Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu kwamba anafanya kazi nzuri.
“Katika hili anastahili pongezi,” amesema Lowassa na kuongeza “Waziri Mkuu yupo kule wengine wapo huku, nchi inawaka moto.”
Lowassa aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kushika nafasi ya pili amesema, juhudi za kiongozi huyo wa nchi anaifanya nchi kushika adabu.
Miongoni mwa mambo anayoeleza Lowassa kwamba yamemvutia katika uongozi wa Rais Magufuli ni kuwaondoa watumishi wasiowajibika vizuri kwenye utumishi wa umma.
Katika elimu, Lowassa amesema Rais Magufuli ameboresha elimu ambayo itawapa ujuzi na kuwawezesha kubuni ili vijana hao waweze kujiajiri.
Tarehe 1 Machi 2019, Lowassa alitangaza kurejea Chama cha Mapinduzi (CCM).
Leave a comment